JAMII YATAKIWA KUSHIRIKI MAPAMBANO DHIDI YA UKATILI WA KIJINSIA


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imeitaka jamii ya kitanzania kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia katika maeneo yao.
 
Hayo yamebainika jana jijini Dodoma katika kikao kilichokutanisha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Wizara ya Afya- Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii na Shirika la UNFPA kilicholenga kujadili jinsi ya kukomesha vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii.
 
Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Stanslaus Nyongo amesema vitendo vya ukatili wa kijinsia vinatokea katika jamii na hivyo Jamii inawajibu wa kukomesha vitendo hivyo.
 
Ameongeza kuwa elimu inahitajika kwa kiasi kikubwa kwa jamii katika kuhakikisha inabadili mitazamo ambayo kwa kiasi kikubwa inasababisha vitendo vya ukatili wa kijinsia katika familia na jamii
 
“Tukifanikiwa kubadili mitazamo ya jamii zetu katika baadhi ya mambo hasi itasaidia sana kupungua kwa vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii zetu” alisema Mhe. Nyongo
 
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Godwin Mollel amesema kuwa Serikali inashirikiana na wadau mbalimbali likiwemo shirika la UNFPA katika kuhakikisha inawafikia jamii hasa za vijijini katika kuwapatia elimu katika midahalo na mikusanyiko  mbalimbali kuhusu madhara ya vitendo vya ukatili kwa ustawi wa jamii
 
Naibu Waziri Dkt. Mollel ameongeza kuwa vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii zetu vinatokana malezi na makuzi ndani ya Jamii.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments