HOSPITALI ZATAKIWA KUWAHUDUMIA MZEE IPASAVYO


 Na.WAMJW-Dsm
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Afya)Prof. Abel Makubi ameziagiza Hospitali zote za Rufaa nchini kuhakikisha wazee wote wanaoenda katika Hospitali hizo kutibiwa , wanapatiwa huduma bora kuanzia anapowasili hospitalini hapo, kwenye Vipimo hadi kwenye kupatiwa dawa, kwani jambo hilo linafahamika na kisera.

Prof. Makubi ametoa agizo hilo wakati wa ziara yake katika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa- Mwanyamala Jijini Dar es salaam wakati wa ziara yake ya kujionea Hali ya utoaji wa huduma Kwenye hospitali hiyo

Amesema pamoja na kuweka waratibu watakaosimamia matibabu ya wazee Kwenye hospitali hizo, kila hospitali ni lazima ihakikishe inaweka wahudumu maalumu watakaowahudumia wazee kuanzia getini na kuwaelekeza maeneo yote ambayo wanaweza kupatiwa huduma bila kupata usumbufu wa aina yoyote ile.

“Wazee wetu ni lazima wapate huduma bora, kuanzia kumpokea, kumpeleka eneo la kupata huduma, kwenye vipimo, hadi kwenye dawa au kama anaenda kulazwa hadi anapotoka, kwa hiyo kwa wazee naomba tusicheze nao, haya ni maelekezo na lazima yatekelezeke” Alisema Prof Makubi.

Katika Hatua nyingine Katibu Mkuu Prof. Makubi amesema ishu ya Fomu ya polisi ya kuthibitisha Matibabu (PF3) isiwe kipingamizi cha mwananchi aliyepata ajali kushindwa kupata huduma ya dharura kwa sababu ya fomu hiyo, na hivyo kuviagiza vituo vyoye vya kutolea huduma ya afya na Hospitali kuhakikisha utaratibu wa PF3 uandaliwa wakati mgonjwa au majeruhi akiwa anapatiwa matibabu.

Prof Makubi amesema ni jambo la kushanganza mwananchi anakosa huduma ya matibabu ya dharura kisa amekosa PF3, hivyo wahusika waandae utaratibu mzuri na Jeshi la Polisi unaotakiwa kufuata ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za dharura bila kero ya aina yoyote.

“Kuanzia sasa vituo vyote vya kutolea huduma nisije nikasikia mtu anakosa huduma aliyepata ajali kwa sababu ya PF3, naomba tulitekeleze hili, utaratibu wa PF3 naomba uandaliwe wakati mtu akiwa anapata huduma.”Alisisitiza Prof. Makubi.

Kuhusu suala la kuzuia maiti kwa baadhi ya Hospitali nchini kutokana na kushindwa kulipa madeni ya matibabu Katibu Mkuu huyo amesema jambo hilo lilishatolewa maelekezo tangu awamu iliyopita na kilichobaki na kuendelea na utekelezaji wa maelekezo hayo. Kama Kuna marehemu anadaiwa,Hospitali ziweke utaratibu mwingine wa ndugu kushirikishwa mapema na kufikia muafaka bila usumbufu.

Prof. Makubi aliongeza kuwa hakuna mtu anayeruhusiwa kuzuia maiti kisa madeni, na wala sio utaratibu wetu Watanzania lakini aliwaomba Wananchi kutoa ushirikiano Kwa Hospitali Kwa kuchangia gharama za huduma za wagonjwa wao mapema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali ya Mwananyamala Bi. Anna Maembe amesema kwa sasa hospitali hiyo imebadilika kwa kiasi kikubwa katika utoaji wa huduma za afya kutokana na maboresho ambayo yamefanywa na Serikali hata hivyo amemuomba katibu Mkuu kuweza kuendelea kushiriana na Hospitali hiyo kuendelea kutatua changamoto zinazoendelea kuikabili ili waweze kutoa huduma iliyo bora kwa wananchi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments