GARI YATUMBUKIA MTONI NA KUUA WATU WANNE NJOMBE


Watu wanne akiwemo Mkuu wa Chuo cha Uuguzi Lugarawa, Steven Mtega (39), wamefariki dunia kwa kuzama kwenye mto Lupali wakiwa kwenye gari waliyokuwa wakisafiria katika Kata ya Lugarawa wilayani Ludewa mkoani Njombe.

Akizungumza kwa njia ya simu Mganga Mkuu wa wilaya ya Ludewa Dkt Stanley Mlay, amesema tukio hilo limetokea Febuari 27 majira ya usiku marehemu hao walikuwa kwenye gari aina ya Toyota Harrier ambapo walikuwa Lugarawa kwenye mambo yao ya mapumziko.

"Walipata ajali kwenye mto Lupali huu mto sasa hivi una maji mengi kwa sababu ya mvua zinavyonyesha, walikuwa watu wanne kwenye mambo yao ya mapumziko Lugarawa na dereva alikuwa huyo mkuu wa chuo wakasema wabadilishe maeneo waende Mundindi sasa walivyofika maeneo hayo ndio wakaingia mtoni," ameeleza Mganga Mkuu Dkt. Mlay.

Dkt. Mlay amewataja marehemu wengine kuwa ni Marko Mpete, fundi umeme wa Lugarawa, Merk Mwalongo (35) mjasiriamali na Rukia Mfaume (28), ambaye alikuwa mhasibu wa mradi wa umeme wa Akra Lugarawa, na miili yao imehifadhiwa katika hospitali ya Lugarawa.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Lugarawa Erasto Mhagama, akizungumzia kutokea kwa tukio hilo amesema tukio hilo limetokea mpakani mwa kijiji cha Shaurimoyo na kijiji cha Amani.

Via>>EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments