WANAODAIWA KUWA MAJAMBAZI SUGU WAKAMATWA TANGA


JESHI la Polisi Mkoani Tanga limewakamata  watu wanne wanaodaiwa kuwa ni Majambazi  sugu waliokuwa wakitafutwa kwa muda mrefu katika wilaya ya Korogwe akiwemo kiongozi  wa genge  la  uhalifu katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Tanga na nje ya mkoa na mlinzi wa kampuni ya Gomba Estate.

Watu hao wanaodaiwa kuwa ni Majambazi wamekamatwa mwishoni mwa wiki katika oparesheni ya Kikosi maalumu cha jeshi la polisi iliyofanyika usiku wa kuamkia Januari 25 katika eneo la kibaoni Mombo wilayani Korogwe .

Akizungumza leo na waandishi wa Habari Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga Blasius Chatanda alisema watu hao wamekamatwa kutokana na Oparesheni ya iliyokuwa ikifanywa na kikosi maalumu cha Jeshi hilo iliyofanyika usiku wa kuamkia Januari 25 katika eneo la kibaoni Mombo wilayani Korogwe
 
aliwataja watu  hao kuwa ni pamoja na Hamis Mbelwa (46),Haji Semkondo,(42), wengine ni Barnaba Simon (62)na Ally Babiwi wote ni wakazi wa Wilaya ya Korogwe.

Akifafanua sifa za watu hao waliotafutwa kwa muda mrefu alisema majambazi wote wamekuwa wakifanya uhalifu wakutumia silaha,

"Kwa mfano huyu Hamis Mbelwa alikuwa ni mfungwa katika gereza kuu la mkoa wa Tanga Maweni na alihukumiwa miaka 30 jela mwaka 2015 katika hukumu iliyotokana na kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha huko Korogwe na alitoroka gerezani na kuungana na genge lake la uhalifu Juni 2019",  Alisema Chatanda.

Aliongeza kuwa kiongozi huyo wa genge baada ya kutoroka Gerezani mwezi Agosti 2019 aliongoza genge lake kufanya uporaji wa kutumia silaha hospitali ya Rosmin iliyopo wilayani Korogwe na kufanikiwa kupora Shilingi milion 8.0.

Akizungumzia  Barnaba Simon Maarufu kwa jina la Nyau spos, Chatanda alisema amekuwa ni mlinzi kampuni ya Gomba Estate iliyopo wilayani Korogwe lakini pia ni mshirika wa genge la uhalifu lililokuwa likiongozwa na Hamis Mbelwa.
 
Alisema kwamba wamekuwa wakitumia silaha aina ya Shotgun yenye usajili  wa 328932 silaha ambayo hutumika kwenye matukio mbalimbali ya uhalifu,

"Huyu ni mlinzi lakini pia ni mshirika wa genge la uhalifu la Hamis Mbelwa na amekuwa akiwakodishia silaha majambazi wenzake kwa ajili ya utekelezwaji wa uhalifu",alisema Chatanda

Alisema wengine Haji  Semkondo na Ally Juma ambao waliokuwa ni washirika wa genge hilo nakwamba wamekuwa wakifanya uhalifu kwa kutumia silaha hususani utekaji barabarani katika  Barabara kuu ya Tanga -Arusha na unyang'anyi wa kpikipiki .

Chatanda alisema msako wa kuwatafuta wahalifu wengine unaendelea  ili kuwakamata wengine waliosalia na watuhumiwa wengine ambao watakuwa wakijihusisha na uhalifu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments