MAENEO YENYE MIFUMUKO YA MADINI LAZIMA YARASIMISHWE - PROF. MANYA

Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya akingumza jambo na baadhi ya wadau wa Madini pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Simiyu.

 Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya katikati, kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka na kulia ni Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula  wakiwa kwenye kikao kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo

Baadhi ya wadau wa Sekta ya Madini wakifuatilia kikao cha Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya.
Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya akitoa ufafanuzi mara baada ya kikao baina yake na wadau wa madini.
Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya akitoa ufafanuzi mara baada ya kikao baina yake na wadau wa madini.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula akizungumza jambo katika kikao cha Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya, kushoto ni Naibu Waziri wa Madini Prof. Manya


Jengo la Kituo cha Umahiri la Mkoa wa Simiyu

Na Tito Mselem Simiyu,

Imeelezwa kuwa mfumuko wa madini (Rush) ni dharura tu, lazima sehemu zote zenye mifumuko ya madini zirasimishwe ili maeneo hayo yaweze kuchangia maduhuli ya Serikali.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya kwenye kikao baina yake na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa huo.

Prof. Manya amesema mfumuko wa madini ni kitu cha mpito hakitaachiwa kiendelee kwa muda mrefu na badala yake kirasimishwe ili kisadie kwenye ushirikishwaji wa watanzania kwenye rasilimali ya madini ambayo watanzania wote wanatakiwa kunufaika nayo.

“Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli alisema wachimbaji wadogo watafutiwe maeneo ya kuchimba ila lazima wazingatie taratibu na sheria ikiwa ni pamoja na kuwa na leseni ya uchimbaji madini husika”, alisema Prof. Manya.

Prof. Manya aliongeza kuwa, Mkoa wa Simiyu umebarikiwa kuwa na madini mbalimbali ikiwemo madini ya metali kama dhahabu, shaba na nikeli, madini ya ujenzi kama mawe, kokoto, moramu na mchanga, madini ya vito kama amethyst na madini ya viwandani kama chokaa na chumvi.

Aidha, Prof. Manya amesema baadhi ya wachimbaji na wadau wengine wa shughuli za madini hawaelewi vyema Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na Marekebisho yake ya mwaka 2017 kuhusu haki ya leseni ya madini na haki ya ardhi hivyo kupelekea wamiliki wa ardhi kutowaruhusu waliopewa haki ya leseni madini kutofanya makubaliano ya fidia katika maeneo yao na kupelekea shughuli za uchimbaji kutofanyika katika maeneo yaliyotolewa leseni.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula amesema Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini imeshafanya mazungumzo na baadhi ya mabenki ili wapatiwe mikopo wachimbaji wadogo wa madini na kuwatoa hofu ya kwamba wachimbaji wadogo hawakopesheki.

“Tuliziambia taasisi za kibenki kwamba wale ambao wana leseni hai wakopeshwe, hivyo wachimbaji wanapaswa kujiunga ili wapatiwe leseni na waondokane na mfumo walionao wa mifumuko ya madini ambapo wanachimba bila leseni, lazima leseni zitolewe na Rush zikome mara moja”, alisema Prof. Kikula.

Naye, Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Mhandisi Yahya Samamba, amewataka wachimbaji wa mkoa wa Simiyu kupendana na kuachana na wivu, majungu, chuki na fitina na badala yake wachimbe kwa kushirikiana ili walete tija kwenye shughuli zao.

Pia Mhandisi Samamba amewapongeza watumishi wa Ofisi ya Madini ya Mkoa wa Simiyu kwa kuvuka lengo la makusanyo ya maduhuli ya Serikali ambapo walipangiwa wakusanye kiasi Tsh milioni 250 na badala yake wamekusanya Tsh bilioni 2.3 ambapo wamevuka lengo kwa zaidi ya asilimia 1700 ndani ya miezi sita.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments