MSIGWA AAHIDI NEEMA JIMBO LA IRINGA MJINI KAMA AKIPEWA RIDHAA YA KUWA MBUNGE TENA

Na Fredy Mgunda,Iringa.
Mgombea ubunge wa jimbo la Iringa Mjini kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Mchungaji Peter Msigwa amewaomba wananchi wa jimbo hilo kumpa miaka mitano mingine ili aendelee kuleta maendeleo kama alivyofanya kwenye miaka kumi ya ubunge wake.

Akizungumza kwenye mkutano wa kuomba kura kwa wananchi wa kata ya Igumbilo Msigwa alisema kuwa Iringa ya sasa imepiga hatua kimaendeleo baada ya kufanya kazi kubwa ya kimaendeleo kama kuboresha sekta ya afya na miundombinu.

Alisema barabara nyingi za jimbo la Iringa Mjini zimejengwa kwa kiwango cha lami kutokana na juhudi za kujenga hoja bungeni na kwa wadau mbalimbali ambao walisaidia kujenga barabara hizo.

"Mnakumbuka nilipoingia madarakani asilimia kubwa barabara zetu zilikuwa za vumbi hivyo nilijitahidi kupambana kuhakikisha kuwa Iringa Mjini inakuwa na miundombinu bora ya barabara",alisema Msigwa

Msigwa aliongeza kuwa wamefanikiwa kuboresha sekta ya afya tofauti na ilivyokuwa awali na ameahidi kuboresha sekta ya afya kwa kutoa bima za afya kwa wananchi wote kwa kuwa ndiyo Sera ya CHADEMA katika uchaguzi wa mwaka huu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527