WANAWAKE WATAKIWA KUTOKUBALI KUTUMIWA NA WANASIASA KUVURUGA AMANI


Na Mwandishi Wetu, Dodoma.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge,Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama amewaasa wanawake kutokubali kutumiwa na vyama vya siasa kama mawakala.


Waziri Mhagama ametoa wito huo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na umoja wa wanawake viongozi wa vyama vya siasa nchini katika mkutano baina yake na viongozi hao uliombatana na hafla ya kumpongeza kwa namna alivyoongoza na kuimarisha vyama vya siasa kwa  kuhakikisha kumekuwa  umoja na mshikamano. 


Mhe.Mhagama amekutana na Viongozi wanawake kwa lengo la kumpongeza kwa kusimamia vema vyama vya siasa ambapo wizara yake ndio inayohusika na usimamizi wa vyama vya siasa kupitia Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini. 


Waziri Mhagama amesema wanawake wana nguvu kubwa na uwezo wa kuwa viongozi na ndio maana Rais Dk John Magufuli amewaamini katika nafasi mbalimbali na hata wakati alipoteuliwa na chama chake kuwa mgombea Urais wa CCM alimchagua tena Mama Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea mwenza wake kwa mara pili. 


” Nguvu yetu wanawake ni kubwa sana na kipindi hiki tunapoelekea kwenye uchaguzi nitoe rai kwenu kugombea nafasi za Uongozi kupitia vyama vyenu, chukueni fomu mkachuane kwenye majimbo na kata msiogope kwa sababu uwezo tunao”amesisitiza 


Tusikubali kusubiri nafasi za upendeleo kama tuna lengo la kufikia 50/50 basi inatulazimu pia tuingie kwenye uwanja wa mapambano ili tupime nguvu zetu, na kwa sababu sisi tuna uwezo mkubwa basi naamini tutashinda,” Amesema Mhagama.

Kwa upande wake Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Francis Mtungi amemshukuru Waziri Mhagama kwa uvumlilivu alionao hali iliyosaidia katika kuratibu zoezi zima la kuimarisha umoja na mshikamano miongoni mwa wanasiasa bila kujali itikadi za vyama vyao. 


Aidha Jaji Mutungi amewataka viongozi hao kutoruhusu kuwa sehemu ya machafuko yanayosababishwa na baadhi ya wanasiasa wasio na uzalendo wa Nchi yao. 


Akizungumzia hoja aliyoitoa Mhe. Rais yakuwa kutakuwa na uchaguzi huru na wa haki, Jaji Mutungi ameongeza kuwa siyo tukwamba uchaguzi utakuwa huru na wa haki unapaswa kumalizika kwa Amani pia kama ambavyo imekuwa desturi ya nchi yetu hivyo amewataka wanawake hao viongozi kuwa chachu ya kusimamia Amani na utulivu wtunapoelekea katika Uchaguzi Mkuu katika maeneo yao.

” Niwapongeze kwa Umoja wenu huu kama viongozi wanawake, mmekuja hapa pamoja mkiwa mmevaliwa sare moja ambayo siyo ya vyama vyenu, niwasihi Umoja huu huu ndio muende nao kwenye uchaguzi mkiweka mbele maslahi ya Nchi yetu,” Amesema Jaji Mutungi. 


Awali  Mratibu wa wanawake viongozi wa vyama  ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha UDP,Bi. Saumu Rashid amemshukuru Waziri Mhagama kwa kukubali kupokea zawadi yao na kumpongeza kwa namna ambavyo amevilea vyama vya siasa kwa muda wote wa miaka mitano.

” Tunakupongeza sana Waziri kwa ushirikiano mkubwa ambao umetupatia, hakika umekua mwema kwetu na tunakuombea urudi bungeni, sisi kama viongozi wanawake tunakuahidi tutakua mstari wa mbele kuchochea amani na utulivu kwenye uchaguzi mkuu,” Amesema Saumu. 


Mwisho. 
 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527