WANAWAKE WATAKA KUUZA ALIZETI YAO KAMA BIDHAA BADALA YA MALIGHAFI


Viongozi na wajumbe wa kikundi cha Mkombozi na Tumaini wakionesha alizeti
Na Sumai Salum- Meatu

Vikundi vya wanawake vya Tumaini Group na Mkombozi Group vilivyopo kata ya Sakasaka wilayani Meatu mkoani Simiyu wamesema hawatauza tena alizeti kama malighafi bali watauza kama bidhaa kutokana na tathmini walizoziona kwenye zao hilo.


Hayo waliyabainisha wakati wanapoendelea na maandalizi maonesho ya Nane Nane yanayotarajia kufanyika kwa mwaka wa tatu sasa kama ilivyo agizo la serikali katika mkoa wa Simiyu ifikapo Agosti 8 mwaka huu.

Walidai kuwa kuuza malighafi kumewachelewesha kufikia malengo ya kundi hilo pamoja na maendeleo ya mtu mmoja mmoja kwani wamekuwa wakipata pesa kidogo ukilinganisha na mafuta ya zao hilo.

“Tumekusudia tuuze alizeti zetu baada ya kuchakata mafuta na kwa gunia moja linatoa lita 17 za mafuta na ukiuza unapata shilingi 60,000/= au 55,000/=/= na ukiuza alizeti bila kusindika unapata 30,000/= ambayo ni hasara kwa mkulima na kikundi, kwa gunia zetu 12 kikundi kitapata faida kubwa itatusaidia kusomesha watoto na maandalizi ya mashamba kwa mwakani” alisema Bi. Christina mhasibu wa Mkombozi Group

“Mradi huu wa alizeti tuliofadhiliwa na REDESO umetupatia manufaa kwani mwaka jana tulipouza mafuta ya alizeti pesa zile zilitusaidia wanakikundi kwani tulikopeshana kwa lengo la kuanzisha miradi ya mtu binafsi wakati tusipokuwa na alzeti tukakopeshana pesa kila mtu 50,000 kwa liba ya 10% wapo waliolima pamba,karanga na hata mahindi pia na vinatusaidia”,alisema Mwenyekiti kikundi cha Tumani Bi.Elizabeth Bisha.

Mbali na hayo, Afisa maendeleo ya jamii kata ya Sakasaka wilayani Meatu mkoani Simiyu Bi. Mbuke Jaulula aliwataka akina mama wakulima wa vikundi vilivyoko katika kata hiyo kuendelea kuwapa wanawake na wanajamii wengine elimu juu ya ulimaji wa zao la alizeti licha ya kuwa linasitahimili ukame bali pia ni zao lenye faida kwa kutoa mafuta na hata chakula cha mifugo lakini pia kwa mwezeshaji wa kikundi hicho ambaye ni REDESO apate mrejesho mzuri dhidi ya matarajio yao wanayoyategemea baada ya kuwawezesha wanakikundi.

“Mwaka huu tumewezeshwa na REDESO mbegu bora za alizeti kwa vikunndi vinne na tumevuna gunia 2 hadi 3 kwa hekali kwa magunia ya debe 6 na tutanufahika pakubwa hivyo niwasihi wanajamii wa kata ya sakasaka hasa wanawake wa jamii hii ya kisukuma kwa kuwa bado kuna mila kandamizi, kupitia kilimo hiki tuwe na amasa zaidi ya ufugaji wa kisasa ikilinganishwa na kuwa tunaishi pembezoni mwa hifadhi na kukosa sehemu ya malisho kwa kulima zao hili tutapata chakula cha mifugo pia na hawatahangaika”aliongeza Bi. Jaulula.

Kwa upande wake Mratibu miradi na Meneja kutokea asasi isiyokuwa ya kiserikali REDESO inayofanya kazi wilayani Kishapu mkoani Shinyanga na baadhi ya kata za wilaya ya Meatu mkoani Simiyu Bw. Charles Buregeya amewapongeza wanakikundi hao huku akiwataka wasiridhike kwa mavuno hayo bali waendeleze bidii na jitihada katika uzalishaji ili waweze kufikia angalau gunia 7 hadi 8 kwa hekali moja kama inavyoshauliwa kitaalamu.

“Lakini pia kijasiriamali mmeonesha ukomavu kwani kuuza alizeti peke yake hautapata tija ukilinganisha na mafuta ila ninachotaka mkizingatie ni kuhakikisha mmeboresha uzalishaji,usindikaji na vifungashio ili tuweze kuingia kwenye ushindani na pia tuhakikishe tunatafuta masoko ili tuweze kuingia kwenye soko la ushindani, na pia shukrani kwa serikali kupitia maendeleo ya jamii kwa ushirikiano wanaotupatia”,alisema Buregeya.
Viongozi na wajumbe wa kikundi cha Mkombozi na Tumaini
Mratibu miradi na Meneja kutoka asasi isiyokuwa ya kiserikali REDESO inayofanya kazi wilayani Kishapu mkoani Shinyanga na baadhi ya kata za wilaya ya Meatu mkoani Simiyu Bw. Charles Buregeya akizungumza
Afisa maendeleo ya jamii kata ya Sakasaka wilayani Meatu mkoani Simiyu Bi. Mbuke Jaulula akizungumza
Afisa maendeleo ya jamii kata ya Sakasaka wilayani Meatu mkoani Simiyu Bi. Mbuke Jaulula na Mratibu miradi na Meneja kutoka asasi isiyokuwa ya kiserikali REDESO inayofanya kazi wilayani Kishapu mkoani Shinyanga na baadhi ya kata za wilaya ya Meatu mkoani Simiyu Bw. Charles Buregeya wakipiga picha ya pamoja na viongozi wa vikundi vya Mkombozi na Tumaini

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527