KATIBU TAWALA KIBAHA: TAULO ZA KIKE MASHULENI NI MUHIMU KATIKA MAHUDHURIO YA WASICHANA

Katibu Tawala wa Wilaya ya Kibaha Sozi Ngate akizungumza katika uzinduzi wa mradi wa ushirikiano wa Mashirika ya Umma na Binafsi katika usimamizi wa Afya ya Hedhi Mashuleni uliofanyika katika Shule ya Sekondari Bundikani wilayani Kibaha.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) Dkt.Ndekya Oriyo akizungumza kuhusiana mradi wa hedhi salama mashuleni na utafiti uliofanyika kwa kupata matokeo.
Mkuu wa Shule wa Sekondari ya Bundikani Bernard Muenjwa akizungumza kuhusiana na upatikanaji wa taulo za kike mashuleni.
Mwanafunzi wa Kidato cha Tatu Shule ya Sekondari Bundikani Saada Shabani akitoa namna watoto wakike wanavyoshindwa kuhudhuria shule wakati wa Hedhi.
Picha ya pamoja watendaji wa NIMR na Kampuni Kasole Secret.
Picha ya pamoja baadhi ya wanafunzi wa kike wakiwa na pakiti mbili za taulo kwa ajili ya Hedhi salama walizogaiwa bure.

Na Chalila Kibuda, Michuzi TV
UPATIKANAJI wa Taulo za Kike ni muhimu kwa maudhurio ya mtoto wa kike shuleni katika kuwawezesha wanafunzi wa kike kuhudhuria shule kikamilifu na kupata haki msingi ya elimu sawa na vijana wa kiume.

Hayo ameyasema Katibu Tawala wa Wilaya ya Kibaha Sozi Ngate wakati wa uzinduzi wa mradi wa ushirikiano wa Mashirika ya Umma na Binafsi katika usimamizi wa Afya ya Hedhi Mashuleni, amesema upatikanaji wa taulo za kike zenye ubora na salama zitawezesha wasichana kupata haki ya elimu na kuwezeza kuchangia lengo namba 3,,4 na 5 la Mkakati ya Maendeleo ya Dunia (SDG’s).

Ngate amesema utafiti uliofanywa na Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) unaonyesha kuwa katika Wilaya 14 za Tanzania Bara ulibaini kuwa asilimia 15 ya wanafunzi wa kike wanashindwa kuhudhuria shuleni wakati wa Hedhi kwa sababu mbalimbali na kato ya hizo asilimia 42 ikichangiwa na ukosefu wa vifaa vya hedhi na asilimia 34 hofu ya kujichafua pamoja na asilimia 26 ni miundombinu ya vyoo isiyo rafiki.

Aidha matokeo ya utafiti wa awali uliofanywa na NIMR na kampuni ya Kasole Secret unaonyesha kuwa asilimia 22 ya wanafunzi wa kike wanashindwa kuhudhuria shule kwa sababu ya changamoto ya hedhi na uapatikanaji wa taulo katika shule zilizo katika mradi ni asilimia 54.

Nae Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIMR Dkt. Ndekya Oriyo akizungumza katika uzinduzi wa Ugawaji wa Taulo za Kike Mashuleni uliofanyika katika shule ya Bundikani zikiwakilishwa na shule tano katika Mji Mdogo wa Kibaha amesema NIMR ina majukumu mawili ambapo upande mmoja ni kutekeleza tafiti zinazolenga kuboresha afya za WaTanzania na upande wa pili ni kuratibu na kudhibiti tafiti za Afya zinazofanyika Tanzania. Leo tumefika hapa kwenu kupitia jukumu letu la kutekeleza tafiti.

Dkt. Oriyo amesema NIMR kwa kushirikiana na Kampuni ya Kasole Secrets wameanza utekelezaji wa mradi wa kitafiti uitwao ‘Ushirikiano wa Mashirika ya Umma na Binafsi katika Usimamizi wa Afya ya Hedhi Mashuleni’ ambapo Mradi huo wa kitafiti unafadhiliwa na Serikali ya Canada kwa kupitia Shirika la ‘Grand Challenges Canada ambalo linalofadhili tafiti zenye ubunifu zinazoonekana kuwa zinaweza kuwa na matokeo ambayo yatakuwa endelevu hivyo Mradi huu utatekeleza kwa muda wa miezi kumi na mbili (12) na unaanza katika shule sita (6) za sekondari za Umma katika Halmashauri ya Mji wa Kibaha. Shule hizi ni Bundikani, Pangani, Simbani, Visiga, Mwambisi Forestry na Kibaha Girls. 

Amesema lengo kuu la mradi huu ni kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya Umma na Binafsi (PPP) ili kuboresha usimamizi wa afya hedhi mashuleni, na kuongeza fursa ya upatikanaji wa taulo za kike zenye ubora na salama ili kuwawezesha wasichana kupata haki ya elimu. 

Amesema malengo mengine ya mradi huo kuanzisha klabu za afya mashuleni zitakazoitwa ‘Pamoja Klabu’, kwa ajili ya wavulana na wasichana ambazo zitatoa elimu kuhusu balehe, hedhi salama na lishe kwa vijana balehe kwa muda wa majuma kumi (10) na kusambaza taulo za kike mashuleni kwa bei ya jumla kupitia utaratibu wa maduka ya shule zinazotengenzwa kampuni ya Kasole Secrets. Taulo hizi zimetengenezwa kwa ubunifu kwa kutumia teknolojia ya mkaa wa mianzi na matumizi ya mkaa wa aina hii na kuonyesha changamoto za kiafya wakati wa hedhi kama vile kuwashwa, fangasi.

Aidha amesema usambazaji wa taulo za kike utafanyika katika awamu mbili. Awamu ya kwanza itahusisha usambazaji wa bure jumla ya paketi za taulo za kike 15,000 zitakazogaiwa katika kipindi cha miezi tatu (3) mfululizo na kila mwanafunzi atapatiwa jumla ya paketi sita (6) na awamu ya pili, itahusisha usambazaji wa taulo za kike kwa bei ya jumla ya shilingi 2,000 chini ya uangalizi wa muda wa miezi tatu (3). 

“Tungependa kufahamisha kuwa awamu ya kwanza ya usambazaji wa taulo za kike bila malipo umeanza na wanafunzi bado wanaendelea kugaiwa ndani ya shule husika”amesema Dkt.Oriyo.

Amesema kabla ya kuanza kutekeleza malengo ya mradi huu, watafiti walifanya tafiti ya awali mwezi Machi, 2020, ambao ulishirikisha wanafunzi 461 wasichana 324 na wavulana 137 na huku lengo lake ilikuwa ni kupima uelewa wa wanafunzi kuhusu masuala ya balehe, hedhi na lishe, na pia kutambua changamoto zinazowakabili wanafunzi wa kike wakati wa hedhi wakiwa shuleni. 

Dkt. Oriyo amesema matokeo ya utafiti wa awali ulibaini uhitaji wa elimu ya balehe na hedhi salama kwa kuwa, ni asilimia 30 tu ya waliohojiwa ambao walionyesha kuwa na taarifa za kutosha, na kati yao asilimia 94 waliomba kupatiwa elimu zaidi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527