DPP AWASIMIMISHA KAZI MAWAKILI WAWILI WA SERIKALI SIMIYU KWA TUHUMA ZA KUWAACHIA HURU WATUHUMIWA SABA WA MAUAJI YA BIBI KIKONGWE


Na Stella Kalinga, Simiyu RS
Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka nchini (DPP),  Bw. Biswalo Mganga amewasimamisha kufanya kazi za mashtaka mawakili wa Serikali mkoani Simiyu, Amani Kirua na Twahab Yahaya kwa tuhuma za kuwaachia huru watuhumiwa saba wa mauaji ya  bibi kikongwe Nchambi Sing’hini  mkazi wa kijiji cha Kinamwigulu wilayani Maswa kinyume na taratibu.

DPP ameyasema hayo Julai 10, 2020 mjini Bariadi wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo pia amemuagiza naibu mkurugenzi wa mashitaka kuwachukulia hatua za kinidhamu haraka; huku akibainisha kuwa mawakili hao hawataenda mahakamani wala kupewa majalada ya mashtaka wakati taratibu za kinidhamu zikiendelea.

“Kuanzia leo mawakili hawa nimewasimamisha kufanya kazi za mashtaka yaani hawataenda mahakamani wala hawatapewa jalada lolote,wakati taratibu za kinidhamu zikiendelea, wakati huo huo jeshi la polisi liendelee kuchunguza kujua ukweli juu ya ‘involvement’ (ushiriki) yao, nakama kuna rushwa na mambo mengine yoyote yamefanyika,” alisema DPP Mganga.

Aidha, DPP Mganga amesema  yapo maelekezo yanayopaswa kufuatwa na mawakili kabla ya  kufuta kesi ambayo ni pamoja na kuandika kwenye jalada sababu zilizofanya kesi ifutwe na mkuu wa mashtaka katika eneo husika kutoa kibali cha kesi kufutwa, ambayo yote yalionekana kutozingatiwa katika ufutaji wa kesi hiyo.

Katika hatua nyingine DPP Mganga amelitaka jeshi la polisi liendelee kuwatafuta watuhumiwa wa mauaji walioachiwa kinyume na taratibu na liwarejeshe mahakamani huku akibainisha kuwa jeshi hilo limeshawakamata watuhumiwa wawili ambao hakuwataja majina kwa sababu za kiupelelezi na watapelekwa mahakamani Julai 13, 2020.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga amesema serikali haitawavumilia watumishi wa umma wanaokiuka taratibu kwa maslahi yao binafsi hivyo itaendelea kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria.

Aidha,  Mmbaga ametoa wito kwa wananchi kuwa na imani na serikali yao na vyombo vyake kwa kuwa mifumo ya serikali ipo na inafanya kazi huku akiwataka kuwa huru kutoa taarifa wakati wowote kupitia vyombo vya ulinzi na usalama.

Mawakili wawili wa Serikali waliosimamishwa kufanya kazi za mashtaka mkoani Simiyu wanatuhumiwa kuwafutia watuhumiwa saba kesi ya mauaji namba moja ya mwaka 2019 ya mauaji ya bibi kikongwe Nchambi Sing’hini,  ambapo alibainika kuwa watuhumiwa wawili walifutiwa kesi hiyo Desemba  31, 2019  na wakili Twahab Yahaya na watano  walifutiwa kesi hiyo  Juni 17 mwaka  huu na wakili Amani Kirua kinyume cha taratibu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527