YANGA, NAMUNGO ZATINGA NUSU FAINALI KOMBE LA SHIRIKISHO


Na Damian Masyenene
Klabu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam imefanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Azam maarufu kama FA baada ya kuichapa timu ya Kagera Sugar ya mkoani Kagera kwa mabao 2-1 katika mchezo wa robo fainali uliochezwa leo kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.


Kagera ndiyo walikuwa wa kwanza kupata bao katika kipindi cha kwanza kupitia kwa kiungo wao, Awesu Awesu ambaye baadae alitolewa kwa kadi nyekundu na Mwamuzi Shomari Lawi, lakini Yanga wakasawazisha katika kipindi cha pili kupitia kwa David Molinga 'Falcao' na Deus Kaseke kwa njia ya Penalti.

Kwa matokeo hayo, Yanga ambayo inatafuta nafasi ya kuiwakilisha nchi kwenye michuano ya kimataifa barani Afrika baada ya kuikosa nafasi hiyo kwenye Ligi, wanasubiri mshindi kati ya Azam FC na Simba SC utakaochezwa kesho Julai 1, 2020 kwenye uwanja wa Taifa Dar es Salaam.

katika mchezo mwingine uliopigwa leo, Wenyeji Namungo FC wamelitumia vyema dimba la nyumbani la Majaliwa Stadium mjini Ruangwa na kufanikiwa kusonga mbele hatua ya nusu fainali ya michuano hiyo baada ya kuinyuka Alliance FC ya Mwanza kwa mabao 2-0.

Ambapo wanasubiri mshindi kati ya Sahare All Stars ya Tanga dhidi ya Ndanda FC ya Mtwara utakaopigwa kesho Jumatano kwenye uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527