11 WAKAMATWA KWA KUWATAPELI WATU KWA KUTUMIA AKAUNTI FEKI ZA FACEBOOK ZA JOKATE MWEGELO, WEMA SEPETU, WOLPER, KAJALA MASANJA


Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kukabiliana na vitendo vya uhalifu na ajali za barabarani ili kuhakikisha kuwa wageni na wakazi wa Mkoa huu wanaendelea kuwa salama na mali zao.


Aidha Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea kushirikiana na wananchi na wadau wengine wa usalama hali inayopelekea kupata mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na kupungua kwa matukio makubwa ya uhalifu pamoja na ajali za barabarani.

KUKAMATWA KWA WATUHUMIWA WA WIZI KWA NJIA YA MTANDAO KWA KUTUMIA AKAUNTI BATILI ZA MITANDAO YA KIJAMII [FACEBOOK].

Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya linawashikilia watuhumiwa kumi na moja [11] ;

1. ALFRED EDIVAI KIGUNGA [22] mkazi wa mtaa wa ZZK – Mbalizi 

2.GEORGE MATHIAS BEMBEJA [24] mkazi wa mtaa wa Kanama – Mbalizi 

3.ELIUD EMIL MAHENGE [24] Fundi rangi, Mkazi wa mtaa wa Kanama – Mbalizi

4. PHILIPO EMANUEL YAWALANGA [22] mkazi wa mtaa wa Ndola – Mbalizi,

5. GASTO GOODLUCK SANGA [21] mkazi wa mtaa wa Tunduma Road – Mbalizi

6. JOHN MICHAEL [21] Mkazi wa ZZK – Mbalizi 

7.EMMANUEL EDWINE @ KALELO [28] mkazi wa Tunduma Road 

8. DAUDI EXAVERY SANGA [23] mkazi wa ZZK Mbalizi 

9. JUNIOR ALLY KAWANGA [21] mkazi wa Songea mkoani Ruvuma 

10. KASTO NEBAT TWEVE [22] mkazi wa Chapakazi Mbalizi na 

11. ALPHA KAYOKA [23] mkazi wa Tarafani Mbalizi 

kwa tuhuma za wizi kwa njia ya mtandao kwa kutumia akaunti batili.

Watuhumiwa walikamatwa kati ya tarehe 21.02.2020 na 22.02.2020 baada ya Jeshi la Polisi Mkoani hapa kufanya msako mkali katika maeneo ya Mji mdogo wa Mbalizi na Jijini Mbeya na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa kumi na moja [11] wanajihusisha na wizi kwa njia ya mtandao kwa kutumia akaunti batili za mtandao wa Facebook zenye baadhi ya majina ya viongozi wa Serikali na wasanii maarufu wa hapa nchini.

Mbinu wanayoitumia wahalifu hao ni kufungua akaunti za “facebook” zenye majina ya baadhi ya viongozi wa serikali na wasanii maarufu na kuuaminisha umma kwa kuweka picha za viongozi na wasanii hao na taarifa zingine kwenye akaunti hizo kisha kuzitumia akaunti hizo kutangaza 

1. Utoaji wa mikopo nafuu

 2. Nafasi za kazi/ajira na 

3. Fursa ya kuendeleza vijana wenye vipaji vya usanii na kuwataka wananchi ambao wapo tayari kutumia fursa hizo kutuma fedha kati ya shilingi elfu ishirini hadi thelathini ikiwa ni bima kwa wanaohitaji mikopo nafuu au gharama ya fomu kwa wanaohitaji ajira. Pia wahalifu hao huweka namba za simu kwa ajili ya wananchi kutuma fedha hizo.

Aidha namba hizo wahalifu huzinunua kwa mawakala wa kusajili laini wasiowaaminifu ambao hutumia namba za NIDA za wateja kusajili laini bila wateja hao kujua na laini hizo kuwauzia wahalifu kati ya Tshs.elfu moja mpaka elfu tano.

Watuhumiwa wamehojiwa na kukiri kufungua akaunti mbalimbali batili za “facebook” za Mh. JOKETI MWEGELO – Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani na akaunti kumi na tatu [13] za wasanii maarufu ambao ni WEMA SEPETU, AUNT EZEKIEL, JACQUELINE WOLPER na KAJALA MASANJA.

Aidha kati ya watuhumiwa kumi na moja [11] wawili ni Mawakala wa kusajili laini kwa kutumia vitambulisho vya NIDA ambao wamekiri kuuza laini hizo kwa wahalifu ambazo wamezisajili kinyume na utaratibu kwa kutumia namba za NIDA za wateja bila wateja hao kufahamu.

WITO WA KAMANDA.
Mosi, natoa wito kwa mwananchi yeyote ambaye amewahi kutuma fedha kwa wahalifu kupitia akaunti hizo batili kufika Makao Makuu ya Polisi Kitengo cha Upelelezi wa Makosa kwa njia ya mtandao [Cyber Investigation], Kituo chochote cha Polisi kilicho karibu yake, Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya kwa ajili ya kutoa taarifa hizo.

Pili, natoa wito kwa wananchi kuwa makini wanapokwenda kusajili laini zao, wasiruhusu namba za vitambulisho vyao vya NIDA kutumika kusajilia laini za watu wengine.

Aidha namna ya kuangalia namba za simu zilizosajiliwa kwa namba za NIDA kama ilivyotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania [TCRA] ni *106# itakupa maelekezo ambayo utachagua option namba mbili [02] ambayo itakupa maelekezo uingize namba ya kitambulisho chako cha NIDA, badae itakupa orodha ya namba za simu zilizosajiliwa kwa kutumia namba ya kitambulisho hicho.

Tatu, natoa wito kwa wananchi kuwa makini na taarifa zinazotolewa kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii ambazo zinaelezea fursa mbalimbali, masomo, biashara na mikopo ambazo zinawataka kutuma kiasi kadhaa cha fedha ikiwa ni moja ya masharti ya kupata fursa hizo, ni vyema kujiridhisha kwenda mamlaka za serikali zilizo karibu kwa ajili ya kujiridhisha kabla ya kufikia hatua ya kutuma fedha.

Nne, nawataka vijana kujenga utamaduni wa kufanya kazi ili kujipatia kipato halali badala ya kujiingiza kwenye vitendo vya kihalifu ambavyo vitawasababishia kupata adhabu kali kwa mujibu wa sheria.

KUKAMATWA KWA WATUHUMIWA WA WIZI WA PIKIPIKI.
Jeshi la polisi mkoani mbeya linawashikiliae watuhumiwa wanne [04] 

1.MASIKITIKO PATSON @ MBUZI [34] Mkazi wa Mtakuja 

2. HURUMA MWASILE [36] 

3. AMANI MSWIMA [21] Mkazi wa Mlima reli na 

4. EZEKIA SINKALA [26] Mkazi wa Mtakuja kwa tuhuma za kuhusika kwenye matukio ya unyang’anyi, uporaji wa Pikipiki katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Mbeya.

Watuhumiwa wamekamatwa mnamo tarehe 12/02/2020 baada ya Jeshi la Polisi Mkoani hapa kufanyika msako maalum maeneo mbalimbali ya Mbalizi na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao. 

Watuhumiwa wote wamehojiwa na kukiri kutenda matukio mbalimbali kama ifuatavyo:-

1. Mnamo tarehe 20/12/2019 majira ya usiku huko Mtakuja mtu aitwaye ZACHARIA JACKSON [30] dereva bodaboda aliuawa kwa kuchomwa na kitu chenye ncha kali kisha kunyang’anywa pikipiki yake aina ya T- BETTER yenye namba za usajili MC 149 CFJ.

2. Mnamo tarehe 10/02/2020 huko MtakujaUtengule Usongwe mtu aitwaye SHUKURU JUMA [26] aliuawa kisha kunyang’anywa pikipiki yake aina King lion.

3. Mnamo tarehe 29/01/2020 huko ZZK Mbalizi majira ya usiku mtu aitwaye SADOCK NIMROD [21] dereva bodaboda alivamiwa na kisha kukatwa na kitu chenye ncha kali shingoni kisha kunyang’anywa Pikipiki.

Upelelezi wa mashauri haya unaendelea na mara baada ya kukamilika watuhumiwa watafikishwa mahakamani.

KUPATIKANA NA MALI ZA WIZI.

Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya linawashikilia watuhumiwa watatu [03]

1. YOHANA MWAIFONGO [33] Mkazi wa Inyala
2. LEONARD SONGOLO [22] Mkazi wa Iyunga na
3. EMMANUEL HAMZA [21] Mkazi wa Iyunga Jijini Mbeya kwa tuhuma ya kupatikana na mali za wizi.

Tukio hilo limetokea mnamo tarehe 27.02.2020 majira ya saa 11:00 asubuhi baada ya Jeshi la Polisi mkoani hapa kufanya msako huko maeneo ya Inyala – Ikuti, Kata na Tarafa ya Iyunga, Jijini Mbeya na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao wakiwa na mali mbalimbali za wizi ambazo ni:-
1. Generator moja ndogo aina ya Tiger.
2. Computer moja aina ya HP
3. Deki moja aina ya Singsung.
4. Speaker ndogo za redio tano aina ya Sea Piano mbili, Aborder mbili na Sansan moja.
5. Sub-Woofer tatu aina ya Sea Piano, Rising na Aborder.
6. Earphone.
7. Printer aina ya Epson.

Watuhumiwa wamefikishwa mahakama ya Mwanzo Iyunga tarehe 27.02.2020 wakihusishwa na matukio mbalimbali CC.NO.70/2020 – Kupatikana na vifaa vya kuvunjia, CC.NO.68/2020 – Kuvunja ofisi usiku na kuiba, CC.NO.69/2020 – Kuvunja kibanda usiku na kuiba, CC.NO.72/2020 – Kuvunja Grocery usiku na kuiba,
CC.NO.106/2020 – Kuvunja nyumba usiku na kuiba.

KUPATIKANA NA MALI ZA WIZI.
Jeshi la Polisi mkoani Mbeya linawashikilia watuhumiwa watatu 

1. CREVA STANLEY [32], 
2. STANLEY GAMASO [23] na
3. OSWARD WESTON [25]
wote wakazi wa Tukuyu kwa tuhuma za kupatikana na mali za wizi.

Tukio hilo limetokea mnamo 01.03.2020 baada ya Jeshi la Polisi kufanya msako Wilaya ya Rungwe na katika upekuzi watuhumiwa walikutwa na mali mbalimbali ambavyo wameiba sehemu mbalimbali hapa mkoani Mbeya. 

Mali walizokutwa nazo watuhumiwa ni:-
1. TV flat screen mbili aina ya Singsung inchi 32 na Samsung inchi 32.
2. Radio moja aina ya Multi Clor VFD Display
3. Mtungi mdogo wa gesi aina ya MIHAN rangi ya njano.
4. Kapeti moja rangi nyekundu.

Watuhumiwa wamekiri kufanya uhalifu maeneo ya Iwambi, Uyole, Forest ya Zamani na Forest Mpya. Watuhumiwa watafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi wa shauri hili kukamilika.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post