WAZIRI MKUU: MUUNDO WA HALMASHAURI YA JIJI LA DODOMA UKAMILISHWE


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameiagiza Ofisi ya Rais–TAMISEMI ishirikiane na mamlaka nyingine, zihakikishe zinakamilisha mchakato wa muundo wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Pia, Waziri Mkuu ameitaka Halmashauri ya Jiji la Dodoma iongeze kasi ya upimaji wa viwanja pamoja na kusimamia kikamilifu udhibiti wa uendelezaji holela wa makazi. “Hatuhitaji kuona Jiji la Dodoma likiwa na makazi yasiyopimwa na holela.”

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Alhamisi, Februari 13, 2020) wakati akizindua mpango kabambe wa jiji la Dodoma katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma.

Waziri Mkuu amesema Serikali haitaki kuona jiji la Dodoma likiwa na makazi yasiyopimwa na holela kwani kasi ndogo ya upimaji wa viwanja kwa halmashauri ya jiji ndiyo itakayosababisha wananchi kujenga makazi holela yasiyopimwa.

Amesema wananchi hawawezi kuisubiri halmashauri bali halmashauri ndiyo inapaswa kuendana na kasi ya mahitaji ya wananchi. “Tayari katika baadhi ya maeneo wananchi wameanza na wanaendelea kujenga bila kufuata taratibu zinazotawala masuala ya ujenzi mijini.”

Waziri Mkuu ameongeza kuwa upimaji wa maeneo uende sambamba na uendelezaji wa miundombinu na huduma muhimu katika maeneo, ikiwemo maji na barabara. “Kasi ya uboreshaji barabara za mitaa iongezwe.”

Pia, Waziri Mkuu amesema halmashauri ya Jiji la Dodoma iweke utaratibu mzuri wa ufuatiliaji, utekelezaji na tathmini ya Mpango Kabambe ili kuhakikisha mpango huo unatekelezwa kikamilifu.

“Hili ni takwa la kisheria kwa mujibu wa kifungu namba 14(3) cha Sheria ya Mipango Miji ya Mwaka 2007 ambacho kinaitaka kila mamlaka ya upangaji kutoa taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kabambe kila mwaka katika maeneo yao ya upangaji kwa Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi.”

Hata hivyo, Waziri Mkuu ameiagiza halmashauri ya Jiji la Dodoma ianzishe mchakato wa kutambua nyumba zote zilizojengwa kwenye barabara kwa lengo la kujua idadi kamili, uhalali wao kuwepo au kama ni wavamizi na baadaye kuandaa utaratibu wa fidia kwa wananchi wanaostahili.

Kadharika, Waziri Mkuu ametoa wito kwa viongozi wa Mkoa wa Dodoma, Wizara, Halmashauri, Taasisi, sekta binafsi, Jumuiya za Kimataifa, wananchi na wadau wengine kuendelea kutoa ushirikiano katika utekelezaji wa Mpango Kabambe ili kufikia malengo ya kuwa na jiji bora, lenye mandhari ya kuvutia na litakalokidhi mahitaji ya kijamii na kiuchumi ya sasa na ya baadae.

Uamuzi wa kuhamishia shughuli za Serikali Dodoma ulifanyika mwaka 1973 ikiwa ni maelekezo ya Chama cha TANU kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa utawala wa awamu ya kwanza chini ya Uongozi wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

 (mwisho)
IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527