Breaking : WATU 20 WAFARIKI DUNIA WAKIGOMBANIA MAFUTA YA UPAKO KWENYE IBADA YA MAHUBIRI YA MTUME 'BULDOZA'



Watu 20 wamefariki dunia leo jioni Jumamosi Februari 1,2020 katika ibada ya mahuburi wakati wa harakati za kukanyaga mafuta ya upako kwenye kongamano la Mtume Boniface Mwamposa 'Buldoza' katika Viwanja vya Majengo Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro.

Inadaiwa kuwa waumini hao walikumbwa na maafa hayo wakati wakikanyagana kwa ajili ya kugombania kukanyaga mafuta yaliyomwagwa na mhubiri huyo yakidaiwa kuwa na upako.
Inaelezwa kuwa watu zaidi ya 40 walikanyagana katika harakati za kugombania mafuta ya upako na kukimbizwa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi.

Idadi ya waliokufa huenda ikaongezeka kwa kuwa hakuna taarifa ya ujumla ya majeruhi waliopelekwa katika vituo vya afya vya jirani pamoja na Hospitali ya Rufaa ya KCMC.

Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Kippi Warioba amelithibitisha  leo saa 5:00 usiku kuwa taarifa za awali waumini 20 wamekufa lakini akasisitiza hizo ni taarifa za awali.

“Taarifa za awali tulizonazo ni kuwa ni waumini 20 wamepoteza maisha lakini tunaendelea kufuatilia maeneo mengine ya zahanati, vituo vya afya na hospitali kama kuna watu walipelekwa huko,” amesema Kippi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post