TAKUKURU YAAGIZWA KUCHUNGUZA 'WALIOTAFUNA' FEDHA ZA UJENZI WA CHOO KAHAMA

NA SALVATORY NTANDU
Serikali mkoani Shinyanga imetoa siku tatu kwa  taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) wilaya ya kahama kufanya uchunguzi wa matumizi ya fedha za ujenzi wa choo kipya  cha shule ya msingi Bukondamoyo baada ya kubaini  kutumika vibaya na kusababisha kutokamilika kwa wakati.


Agizo hilo limetolewa febuari 26 mwaka huu na mkuu wa mkoa wa Shinyanga Zainab Telack baada ya kufanya ziara ya kushitukiza katika shule hiyo iliyopo katika halmashauri ya mji Kahama  ili kuona maendeleo ya ujenzi wa choo.

“Nilipata taarifa za upotoshaji  katika mitandao ya kijamii zilizowekwa na watu wasiokuwa na nia nzuri na maendeleo ya shule hii kuwa shule hii haina choo, nimefika ili nijiridhishe nimebaini kamati ya shule hii imetumia fedha za wananchi vibaya katika ujenzi wa choo kipya”alisema Telack.

Telack aliwataka TAKUKURU kuhakisheni wananafanya uchunguzi wa kina ili kubaini ninani alihusika katika matumizi ya fedha za ujenzi wa choo hicho na kuwataka watu wanaosambaza taarifa kuwa shule hiyo haina choo kuacha mara moja kwani serikali tayari imeshachukua hatua za haraka kukabiliana na suala hilo baada ya choo cha awali kubomoka.

“Tayari mkurugenzi wa mji kahama ameshachukua hatua za haraka kwa kuleta vyoo vya dharura (mobile toilet) katika shule hiyo pamoja na kutoa fedha zaidi ya milioni 100 kwaajili ya kukamilisha ujenzi wa vyoo hivyo ili wanafunzi wawezekupata huduma nzuri”alisema Telack.

Awali akitoa taarifa za ujenzi wa choo hicho diwani wa viti maalum wa kata ya bukondamoyo Scholastika Danford alisema kuwa wananchi katika mtaa huo wamegoma kuchangia ujenzi wa choo hicho kutokana na kamati ya shule hiyo kutokuwa wawazi katika ujenzi kwa kushindwa kusoma taarifa za mapato na matumizi.

“Sio kweli wananchi hawataki kuchangia maendeleo tatizo hapa hakuna uwazi shimo pekee la choo hiki linadaiwa kutumia zaidi ya shilingi milioni mbili jambo ambalo linawatia mashaka kuendelea kuchangia ujenzi huu”alisema Danford.

Aliongeza kuwa kamati ya shule hiyo imeshindwa kusimamia ujenzi wa choo hicho jambo ambalo limeilazimu halmashauri ya Mji kahama kuingilia kati kwa kutoa fedha kwaajili ya kujenga vyoo hivyo ili kuwawezesha wanafunzi kupata huduma hiyo baada ya vyoo vya awali kubomoka.

Naye  mwalimu mkuu wa shule hiyo Modesta Kalisius alisema kuwa shule hiyo inawanafunzi 2467 na madarasa 11,matundu sita na uhitaji wa vyoo ni matundu 111.

“Wasichana wanahitaji matundu 61 na wavulana matundu 50 naiomba  halmashauri ya ikamilishe  ujenzi wa choo hiki kwani kilichopo  majengo yake ni chakavu na yamejaa”alisema Modesta

Mwisho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527