BUNGE LA SENETI LAMSAFISHA RAIS TRUMP DHIDI YA MASHTAKA YALIYOTISHIA KUMUONDOA MADARAKANI


Rais Donald Trump wa Marekani ametolewa hatiani dhidi ya tuhuma zilizokuwa zikimkabili za kutumia vibaya madaraka kufuatia uamuzi uliopitishwa na Seneti ya nchi hiyo inayohodhiwa na chama chake cha Republican.

Kikao cha 12 cha kesi iliyokuwa ikimkabili rais wa 45 wa Marekani kilianza jana jioni kwa saa za Marekani katika Baraza la Seneti; na katika siku hiyo ya mwisho ya kesi hiyo maseneta walipiga kura baada ya waungaji mkono na wapingaji wa mpango wa kumuuzulu Trump kutoa maelezo yao.

Katika mchakato wa upigaji kura, maseneta 52 wa chama cha Republican walipinga kumtia hatiani kiongozi huyo mkabala na maseneta 47 wa chama cha Democrat pamoja na seneta mmoja wa Republican ambao walimtia hatiani kwa mashtaka yaliyokuwa yakimkabili.

Trump angeuzuliwa na kuondolewa madarakani endapo maseneta 67, ambao ni sawa na heluthi mbili ya maseneta wote, wangeunga mkono mashtaka yaliyowasilishwa dhidi yake.

Kwa kuzingatia kuwa Seneti ya Marekani inahodhiwa na chama cha Republican chenye wajumbe 53 mkabala na 47 wa chama cha Democrat, ilitarajiwa tokea awali kuwa Trump angetolewa hatiani dhidi ya tuhuma zilizokuwa zikimkabili.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Juu ya Marekani John Roberts ndiye aliyeyatangaza matokeo hayo.

''Katika shauri hili la mashtaka, maseneta 48 wamesema Donald John Trump anayo hatia kwa makosa aliyoshtakiwa, maseneta 52 wamesema hana hatia kwa mashtaka hayo. Waliomkuta na hatia hawafiki theluthi mbili ya maseneta waliopo. Kwa hiyo Rais Donald John Trump hakukutwa na hatia katika shauri hili la mashtaka.'' Amesema Jaji Roberts.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post