NCHI ZA AFRIKA MASHARIKI ZASITISHA SAFARI KWENDA CHINA KUTOKANA NA MLIPUKO WA VIRUSI VYA HOMA YA CORONA


Shirika la Ndege la Kenya (KQ) na Shirika la Ndege la Rwand (Rwandair) yametangaza kusitisha safari zote za kwenda na kutoka China kutokana na mlipuko wa virusi vya homa ya corona.

Virusi hivyo vilivyoenea katika nchi zaidi ya 16 hadi sasa vimepelekea vifo vya watu zaidi ya 200, huku visa vilivyoripotiwa vikiwa takribani 10,000.

Hadi sasa visa sita vya virusi hivyo vimeripotiwa barani Afrika, lakini washtukiwa wote hawakukutwa na virusi hivyo. Januari 28, mwaka huu mwanafunzi mmoja aliwekwa chini ya uangalizi jijini Nairobi, Kenya baada ya kuwasili kutoka mjini Wahun, China eneo virusi hivyo vilipoanzia.

KQ imesema kuwa mazungumzo na wizara ya mambo ya nje na wizara ya afya yanaendelea ili kuweza kuamua urefu wa zuio hicho.

Rwandair katika tangazo lake imeeleza kuwa abiria watakaoathirika na kuzuiwa kwa safari hizi kwa muda, watarudishiwa fedha zao, kupangiwa safari hizo kwa tarehe za mbele ama kubadilishiwa njia.

Aidha, Rwandair imesema safari kati ya Kigali na Mumbai zitaendelea kama kawaida, huku KQ pia ikiendelea na safari zake kwenda Bangkok nchini Thailand.

Wakati KQ na Rwandair wakisitisha safari za China, Shirika la Ndege la Ethiopia Airlines limesema, litaendelea kufanya safari zake za kwenda China, kwani mamlaka za nchi hizo mbili zinafanya kazi kwa karibu ili kuwalinda abiria na wafanyakazi wake dhidi ya virusi hivyo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527