MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA) YATOA TAHADHARI YA MVUA KUBWA


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari kwa wananchi wanaoishi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, Kaskazini na Kanda ya Kati kukumbwa na mvua kubwa kwa siku tano mfululizo. 


Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na mamlaka hiyo, mvua hizo zinatarajia kunyesha katika mikoa ya Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Mara, Kagera, Geita na Tabora kwa Kanda ya Ziwa.

Mikoa ya Kanda ya Kati itakayokumbwa na mvua hizo ni Singida na Dodoma huku mikoa ya Kanda ya Kaskazini ikiwa Kilimanjaro, Arusha na Manyara.

Sambamba na mikoa hiyo, taarifa hiyo ilisema mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ambayo ni Rukwa, Iringa, Mbeya na Njombe pia itakumbwa na mvua hiyo.

Aidha, taarifa hiyo ilieleza kuwa mvua hizo zinatarajia kusababisha uharibifu wa miundombinu na mali kwa baadhi ya maeneo pamoja na makazi kuzungukwa na maji.

"Athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua hizo ni baadhi ya makazi kuzungukwa na maji, ucheleweshwaji wa usafiri na kusimama kwa muda kwa baadhi ya shughuli za kiuchumi na kijamii," ilisema taarifa hiyo.

Kutokana na hatari hiyo, TMA imewatahadharisha wananchi wanaoishi katika mikoa hiyo, kuchukua tahadhari mapema pamoja na kujiandaa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527