TPDC YAOKOA TRILIONI12.7 KUAGIZA MAFUTA NJE YA NCHI


SHIRIKA la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano imefanikiwa kukoa kiasi cha Tsh. Trilioni 12.7 kwa kutumia gesi asilia katika kuzalisha umeme badala ya kutumia fedha za kigeni kuagiza mafuta.

Hayo yamesemwa leo (Ijumaa Desemba 13, 2019) Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt. James Mataragio wakati alipokuwa akitoa taarifa yake kwa waandishi wa vyombo vya habari kuhusu  utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.

Mataragio alisema kwa kutumia gesi asilia tangu mwaka 2004, TPDC imesaidia kuokoa kiasi cha Tsh. Trilioni 30.225 ambazo Tsh. Trilioni 27.6 zingetumika kuagiza mafuta kwa ajili ya kuzalisha umeme au kutumika kama nishati viwandani.

‘’Kwa kutumia gesi asilia kuzalisha umeme au kama nishati viwandani, TPDC imelisaidia taifa kutotumia fedha za kigeni kuagiza mafguta kwa ajili ya kuzalisha umeme au kutumika viwandani, ambapo kwa kipindi cha miaka minne tumeokoa Tsh. Trilioni 12.7’’ alisema Dkt. Mataragio.

Alisema kuwa uzalishaji wa umeme kwa gesi asilia umeongezeka kutoka Megawati 553 mwaka 2015 hadi kufikia Megwati 892.7 mwaka 2019 ikiwa ni ongezeko la asilimia 61, huku asilima 57 ya umeme katika gridi ya taifa ukizalisshwa kwa kutumia gesi asilia, hatua iliyowezesha kuondoa upungufu wa umeme katika kipindi cha kiangazi.

Akiainisha mafanikio mengine, Dkt. Mataragio alisema kati ya kipindi cha mwaka 2016/17 hadi Oktoba 2019, TPDC imechangia kwenye pato la Taifa kiasi cha Tsh. Bilioni 243.05, ambapo matarajio ya ofisi yake ni kuhakikisha kuwa kati ya mwaka 2020/21 hadi 2023/24 TPDC inachangia kiasi cha Bilioni 599.62.

Aidha aliongeza kuwa katika kipindi cha mwaka 2016/17 hadi Oktoba 2019, TPDC imechangia kwenye mfuko wa mafuta na gesi asilia kiasi cha Tsh. Bilioni 120.56, ukiwa ni mfuko maalum ulioanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Petroli ya mwaka 2015, na pia kwa mwaka 2018/19 TPDC imefanikiwa kutoa Gawio kwa Serikali la kiasi cha Tsh. Bilioni 2.5.

Kwa mujibu wa Dkt. Mataragio alisema katika kipindi cha miaka minne kumekuwepo na ongezeko la matumizi ya gesi asilia kwenye magari, ambapo hadi sasa kuna magari 305 yanayotumia gesi asilia katika Jiji la Dar es Salaam na idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka zaidi, ambapo TPDC inatarajia kuweka mikakati madhubuti  ya kufanikisha mpango katika Jiji la Dar es Salaam.

Akitaja mikakati hiyo, Dkt. Mataragio alisema TPDC ipo katika utekelezaji wa kujenga vituo vikubwa viwili vya CNG katika Jiji la Dar es Salaam ambavyo vitawezesha usambazaji wa gesi asilia katika mfumo wa CNG kwa ajili ya magari na  kuwa na vituo vya kujazia gesia asilia katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.

Kuhusu usambazaji wa gesi asilia majumbani, Dkt. Mataragio alisema hadi kufikia Novemba 2019, matumizi ya gesi asilia majumbani katika Jiji la Dar es Salaam imefikia yyumba 73 mwaka na wakati kwa Mkoa wa Mtwara idadi ya nyumba zinazotumia gesi asilia zimefikia 385, ambapo katika bajeti ya mwaka 2019/2020 TPDC imepanga kuunganisha nyumba zaidi ya 1500 kwa Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Mtwara.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527