RAIS MAGUFULI ATANGAZA KUHAMIA DODOMA KUANZIA LEO



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwa amesimama kwenye msari na mke wake Mama Janeth Magufuli pamoja na wananchi wengine wakati wakielekea kujiandikisha katika daftari la Wapiga Kura kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mtaa katika Kitongoji cha Sokoine Chamwino mkoani Dodoma leo tarehe 12/10/2019. Picha na Ikulu
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akijiandikisha katika daftari la Wapiga Kura kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mtaa katika Kitongoji cha Sokoine Chamwino mkoani Dodoma leo tarehe 12/10/2019. Kulia aliyekaa ni Afisa Uchaguzi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Mary Joseph Mwambongo
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akijiandikisha katika daftari la Wapiga Kura kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mtaa katika Kitongoji cha Sokoine Chamwino mkoani Dodoma leo tarehe 12/10/2019. Kulia aliyekaa ni Afisa Uchaguzi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Mary Joseph Mwambongo.


Na Gerson Msigwa, Ikulu


 Rais wa Tanzania, John Magufuli ametangaza kuhamia Dodoma kuanzia leo Jumamosi Oktoba 12, 2019.

Rais Magufuli amesema hayo mara baada ya kumaliza kujiandika katika orodha ya wapiga kura ya serikali za mitaa akiwa na mkewe Mama Janeth Magufuli.

Wawili hao wamejiandika katika kituo cha Sokoine kilichopo katika Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma baada ya kuwasili wakitoka mkoani Katavi.

Baada ya kujiandikisha, Rais Magufuli amesalimiana na wananchi wa Chamwino waliokuwa wamejitokeza kujiandikisha katika kituo hicho na kuwaeleza kuwa pamoja na kwamba miundombinu ya Ikulu ya Chamwino bado haijakamilika yeye ameshahamia Dodoma.

“Mimi nilikuwa Katavi, nimeamua kuja kujiandikisha nyumbani kwa sababu hapa ndio nyumbani kwangu, na nimeshakuja rasmi hapa, kwa hiyo kila siku tutakuwa tunaonana hapa, ndio maana nimeona nije nijiandikishe mimi pamoja na mke wangu” amesema Rais Magufuli.

Uamuzi huo wa Rais Magufuli umehitimisha ahadi yale aliyoitoa huko nyuma ya kuhamia Dodoma kwani tayari Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, wizara na taasisi mbalimbali zilikwisha kuhamia Dodoma.

Kuhusu uchaguzi, Rais Magufuli amewataka Watanzania kuendelea kujitokeza katika vituo vya kujiandikisha vilivyopo nchi nzima ili Novemba 24, 2019 waweze kutumia haki yao ya kikatiba ya kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa watakaowana wanafaa.

Aidha, Rais Magufuli amewapongeza waandishi wa habari wa Mkoa wa Dodoma waliofika katika kituo hicho kwa kutekeleza majukumu yao ya uandishi wa habari na amewasisitiza kuendelea kutimiza majukumu hayo kwa weledi na kwa kutanguliza maslahi ya Taifa.

Baadaye, Rais Magufuli amewaalika waandishi wa habari hao na kula nao chakula cha mchana, nyumbani kwake katika Ikulu ya Chamwino.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527