BALOZI SOKOINE AMUWAKILISHA WAZIRI SIMBACHAWENE KUZINDUA MFUMO WA UKUSANYAJI TAKWIMU ZA GESIJOTO


Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Balozi Joseph Sokoine amezindua Mfumo wa Kitaifa wa Ukusanyaji Takwimu za Gesijoto, Ufuatiliaji, Uandaaji Taarifa na Uhakiki katika Ukumbi wa Kituo cha Kuratibu Hewa Ukaa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA) mkoani Morogoro.

Akizindua mfumo huo kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa ais (Muungano na Mazingira) Mhe. George Simbachawene, Balozi Sokoine alisema kuwa utawezesha nchi kukusanya takwimu za gesijoto kutoka sekta mbalimbali kwa ajili ya kuchukua hatua stahiki na maamuzi.

Pamoja na mambo mengine alisema pia utasaidia kuandaa taarifa mbalimbali ambazo nchi inatakiwa kuandaa kama Mwanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi ambazo zinabainisha kiasi cha uzalishaji wa gesijoto kutoka sekta mbalimbali husika na uondoshaji wake kupitia misitu.

Balozi Sokoine aklibainisha kuwa hadi sasa Tanzania imeandaa taarifa mara mbili na kuwasilisha Sekretareti ya Mkataba mwaka 2003 na ya pili mwaka 2015 na kwa muda wote Tanzania kama ilivyokuwa kwa nchi nyingine.

Aliongeza kuwa Tanzania imetumia wataalamu elekezi kufanya kazi hii chini ya Mradi uliokuwa unatekelezwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kuratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais Idara ya Mazingira hivyo kuleta ugumu katika kuthibiti ubora na kulinganisha takwimu za nchi mbalimbali kwani hakukuwa na mfumo au njia iliyokubalika kimataifa kufanya kazi na haikujenga uwezo wa sekta husika.
"Mfumo wa Kitaifa wa ukusanyaji na usimamizi wa Takwimu za gesijoto, unaozinduliwa leo utawezesha nchi kutoa  takwimu sahihi na za kutosheleza kuhusu uzalishaji wa gesijoto kutoka sekta mbalimbali husika na uondoshaji kwa njia ya misitu, kwa hatua sahihi za uamuzi na kutoa taarifa," alisema.

Aidha Balozi Sokoine alisema kuwa uzinduzi wa Mfumo huu umekuja wakati muafaka ambapo tunajipanga kuanza utekelezaji wa Makubaliano ya Paris ambayo yalipitishwa na Mkutano wa 21 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabinchi na Tanzania kuridhia Mei 2018.

Aliongeza kuwa kwa sasa Tanzania inakamilisha maandalizi ya Mchango wake katika juhudi za kupambana na Mabadiliko ya Tabianchi hivyo Mfumo huo utasadia katika upatikanaji wa takwimu na taarifa kuhusu utekelezaji wa NDCs na uandaaji wa Taarifa ya Tatu ya Mawasiliano.

" Utekelezaji wa Mfumo huu utahitaji kila mdau kubaini majukumu yake na kuyatekeleza na hivyo kila mdau anatakiwa kubaini majukumu yake kama yalivyobainishwa katika Mfumo ili  kuhakikisha kuwa Mfumo huu unatekelezwa na hivyo kutuwezesha kufikia malengo tarajiwa," alisisitiza Balozi Sokoine.

Naibu Katibu Mkuu aliagiza Kituo Cha Kitaifa cha Kuratibu Hewa Ukaa (NCMC) kuratibu na kusimamia mfumo wa Kitaifa wa Ukusanyaji Takwimu za Gesijoto, Ufuatiliaji, Uandaaji Taarifa na Uhakiki.

Aliagiza Wizara za Kisekta ziteue Wataalamu watakaohusika na usimamizi na uandaaji wa takwimu za uzalishaji wa gesijoto katika sekta zao na kuwasilisha kwenye Kituo cha Kitaifa cha Kuratibu Hewa Ukaa.

Pia aliagiza Wizara za Kisekta kwa kushirikiana na Kituo cha Kitaifa cha Kuratibu Hewa Ukaa ziweke Utaratibu wa kuwasilisha taarifa katika Kituo cha Kitaifa cha Kuratibu Hewa Ukaa kila mwaka.na kubainisha watoaji takwimu chini ya sekta zao za uzalishaji wa gesijoto na kuweka utaratibu wa kupata takwimu hizo.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527