UBORESHAJI WA DAFTARI LA WAPIGA KURA KUFANYIKA AGOSTI 26 HADI SEPTEMBA 1, 2019 SHINYANGA



Kamishina wa Tume ya Uchaguzi ya Taifa nchini Tanzania,Mhe. Balozi Omari Ramadhani Mapuri akifungua mkutano wa Tume na Wadau wa Uchaguzi katika mkoa wa Shinyanga kwa lengo la kupeana taarifa kuhusu uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura. Picha na Kadama Malunde - Malunde1 blog

 Kamishina wa Tume ya Uchaguzi ya Taifa nchini Tanzania,Mhe. Balozi Omari Ramadhani Mapuri amesema zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura mkoa wa Shinyanga litafanyika kuanzia Agosti 26,2019 hadi Septemba 1,2019.

"Tume inatarajia kuanza uboreshaji wa daftari la wapiga kura kwa awamu ya nne katika mikoa ya Mwanza (halmashauri ya wilaya Kwimba),mkoa wa Shinyanga na mkoani Geita (Halmashauri ya Mji wa Geita,Nyang'wale,Bukombe na Mbogwe) kuanzia Agosti 26 hadi Septemba 1,2019",amesema Balozi Mapuri.

Amefafanua kuwa uboreshaji wa daftari la wapiga kura unafanyika kwa kutumia teknolojia ya kielektroniki ya Biometriki (BVR) ambayo huchukua taarifa za kibaiolojia za mtu na kuzihifadhi katika Kanzidata(Database) kwa ajili ya utambuzi.

"Uboreshaji wa daftari la wapiga kura wa safari hii hautahusisha wapiga kura walioandikishwa kwenye daftari la kudumu la wapiga kura mwaka 2015 ambao kadi zao hazihitaji marekebisho yoyote ya taarifa.Uboreshaji huu utawahusu wapiga kura wapya ambao wametimiza umri wa miaka 18 na wale ambao watatimiza umri wa miaka 18 siku ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.",amesema Balozi Mapuri.

Amesema uboreshaji huo pia utahusisha watu ambao wamehama kutoka maeneo yao ya awali na kuhamia maeneo mengine ya uchaguzi na wale ambao kadi zao zimeharibika au kupotea na wale ambao wanatakiwa kufutwa kwenye daftari baada ya kupoteza sifa wakiwemo waliofariki dunia.

Amewataka watu wenye sifa ya kujiandikisha wajitokeze kwa wingi ili waandikishwe na wanaohitaji kuboresha taarifa zao wakati ndiyo huu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527