SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WAAJIRI WANAOWANYIMA HAKI WANAWAKE LIKIZO YA UZAZI

 Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- DOMOMA

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya imetangaza kuanza kuwachukulia hatua Waajiri wote ambao wanavunja Sheria kwa kugandamiza haki ya kupata likizo ya uzazi kwa wanawake pindi anapojifungua.

Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya unyonyeshaji Duniani yaliyofanyika katika ofisi za Wizara ya Afya Jijini Dodoma, yenye kauli mbiu ya “Wawezeshe wazazi kufanikisha unyonyeshaji”.

“Haki ya Mwanamke Kuzaa na kupata likizo ya uzazi ni haki yake ya asili, haitakiwi kuwekewa vikwazo au changamoto yoyote, kwahiyo nitoe wito kwa wanawake ambao wanafanya kazi, ni haki yako kupata likizo, asije mtu anakwambia anaijaza kazi yako kwakuwa umetoka likizo ya kujifungua, tuambie sisi, tutachukua hatua, na huyo Mwajiri tutamtangaza kuwa ni adui wa Wanawake na Watoto wa Tanzania “.Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy aliendelea kusema kuwa Serikali ipo katika mpango wa kuanzisha dawati la kutoa malalamiko litaloshughulikia kupigania na kutetea haki za wanawake kupata likizo ya uzazi, jambo litalosaidia kudhibiti tabia za baadhi ya Waajiri kukandamiza haki za wanawake baada ya kujifungua.

Kwa upande mwingine, Waziri Ummy amesema kuwa takribani asilimia 97 ya watoto wenye umri chini ya miaka miwili wananyonyeshwa maziwa ya mama, hii inaonesha kuwa hali ya unyonyeshaji wa maziwa ya mama imepungua ikilinganishwa na takwimu ya mwaka 2015/2016 ambayo ilikuwa ni asilimia 98.

Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa idadi ya watoto wanaoanzishiwa kunyonyeshwa maziwa ya mama kwa wakati sahihi (ndani ya saa moja baada ya kuzaliwa) ni asilimia 53 ikilinganishwa na asilimia 51 ya mwaka 2015/2016

Aliendelea kusema kuwa, idadi ya watoto wanaonyonyeshwa maziwa ya mama pekee bila kupewa maji, vinywaji na vyakula vingine katika kipindi cha miezi sita ya mwanzo baada ya kuzaliwa ni asilimia 58 ikilinganishwa na asilimia 59 ya mwaka 2015/2016.

Hata hivyo, Waziri Ummy amesema kuwa Idadi ya watoto wenye umri wa miezi 6 hadi 23 wanaolishwa chakula kinachokidhi vigezo vya ubora kilishe ni 35%, huku kiwango kikionekana kuongezeka ikilinganishwa na asilimia 10 kwa mwaka 2015/2016.

Mbali na hayo, Waziri Ummy amesema kuwa, takwimu za utafiti wa hali ya lishe nchini za mwaka 2018 zinaonyesha kuwa asilimia 31 ya watoto walio chini ya umri wa miaka mitano wamedumaa ikilinganishwa na asilimia 34 ya mwaka 2015/2016, huku sababu kubwa ya ikiwa ni ulishaji usio sahihi ambao huchangiwa na majukumu mengi yanayomkabili mama na hivyo kukosa muda wa kutosha wa kumtunza mtoto.

Naye Mwakilishi kutoka UNICEF Bw. James Gitau amesema kuwa, unyonyeshaji ni moja ya njia muhimu kuhakikisha Afya Bora kwa maisha ya mtoto, hivyo kutoa wito kwa wanahabari kuhakikisha wanapeleka Elimu kwa wananchi hususan wanawake kuhakikisha wanafahamu umuhimu wa kunyonyesha Watoto mfululizo miezi sita ya mwanzo,

Pia, Bw. James Gitau ametoa wito kwa Serikali kuongeza nguvu katika uhamasishaji juu ya umuhimu na haki ya Watoto kunyonyeshwa, amesema jambo hili litasaidia kuokoa watoto kupata magonjwa yanayotokana na kukosa virutubisho kutoka kwa maziwa ya mama.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527