DANI ALVES AREJEA KWAO BRAZIL


ANAZEEKA na utamu wake kama muwa. Huyo ndiyo Dani Alves, ambaye amemwaga wino wa kuitumikia klabu ya nyumbani kwao Brazil ya Sao Paulo baada ya kumaliza mkataba wake na PSG.

Alves amesaini na miamba hao Brazili mkataba wa hadi Desemba 2022.

Beki huyo wa kulia mwenye umri wa miaka 36 – ambaye alihamia Ulaya kwa mara ya kwanza 2002, aliposajiliwa na Sevilla akitokea Bahia – alikuwa hana timu baada ya kumaliza mkataba wake na PSG baada ya kuitumikia kwa miaka miwili katika Ligi Kuu ya Ufaransa, Ligue 1.

Alves alihusishwa na klabu yake ya zamani ya Barcelona na klabu nyingine za Ligi Kuu ya England, lakini veteran huyo alichagua kurudi nyumbani Brazil wakati akifukuzia kwenda kwenye Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar.

Beki huyo aliiongoza timu ya taifa ya Brazil akiwa nahodha walipotwaa ubingwa wa Copa America kwenye ardhi ya nyumbani Julai – na kufikisha jumla ya makombe aliyotwaa kuwa 40.

Alitangaza kupitia video iliyopostiwa kwenye ukurasa wa Twitter wa klabu ya Sao Paulo, akielezea sababu za kutua katika klabu hiyo aliyokuwa akiishabikia utotoni.

"Ningeweza kuchagua timu yoyote nyingine," Alves alisema. "Lakini nimechagua kurudi Brazil, katika nchi yangu, kwa watu wangu. Kwenye klabu ninayoipenda.
"Ni kama ndoto, lakini niko hapa!"
Chanzo - Mwanaspoti

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527