TANZANIA KUENDELEA KUNUFAIKA KIUCHUMI NA SADC

Na Frank  Mvungi- MAELEZO- Morogoro

Katibu Mkuu Mstaafu Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Mussa Uledi amesema kuwa Tanzania inanufaika kiuchumi  kama mwanachama wa Jumuiya ya Maendeleo  Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na jumuiya nyingine ambazo Tanzania ni mwanachama.

Akizungumza wakati akiwasilisha mada leo mjini Morogoro ikiwa ni siku ya pili ya mafunzo  kwa waandishi  wa habari ya kuwajengea uwezo wa kuandika na  kuripoti   habari za SADC, Bw. Uledi amesema kuwa  nchi yetu imenufaika na utekelezaji wa miradi ya miundomnbinu,  biashara, uwekezaji  na viwanda.

“ Mkakati wa maendeleo wa SADC unafafanana kwa kiwango kikubwa na ule wa Tanzania ambao pia unazingatia haja ya utekelezaji wa viwanda na miundombinu hapa nchini hali itakayochangia katika kuimarisha maendeleo na kukuza uchuni na ustawi wa wananchi” Alisisitiza Bw. Uledi

Akifafanua amesema kuwa vipaumbele vya Tanzania vimejikita katika upanuzi wa Mauzo nje na uongezaji wa michepuo yake lengo likiwa ni kukuza na kuendeleza biashara hali inayowezesha uendelezaji wa viwanda vya kuongeza thamani katika malighafi za ndani hususan mazao ya kilimo na madini.

Aliongeza kuwa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli  katika baadhi ya nchi wanachama wa SADC imeonesha kuwa Tanzania imejipanga vizuri kimkakati inaweza kuwa ghala la Chakula kwa kukuza zaidi uzalishaji kuendana na mahitaji katika soko la jumuiya hiyo na hata nje ya jumuiya.

 Alitaja vipaumbele vingine kuwa ni pamoja na  uendelezaji miundombinu kama barabara, reli, usafiri wa anga, uzalishaji na usambazaji huduma za umeme ambayo ni nyenzo muhimu sana katika kuyaunganisha masoko ya nchi wanachama wa SADC.

Aliongeza kuwa vipaumbele vingine ni utafutaji wa rasilimali na utekelezaji wa miradi ya Kikanda kwa kuundwa kwa kikosi kazi cha Mawaziri wenye dhamana ya Fedha na uendelezaji miundombinu, Amani na Usalama umeendelea kuimarika ndani ya SADC.

Tanzania inatarajiwa kuleta msukumo mpya kwa nchi wanachama wa SADC katika utekelezaji wa miradi na program za maendeleo za Jumuiya hiyo kwa kuwa itakuwa na dhamana kubwa ya kukidhi matarajio makubwa ya nchi wanachama wakati wote wa uenyekiti wake.

Kwa upande wake Mkuu wa Operesheni na Mafunzo, Brigedi ya Magharibi ya Jeshi  la Ulinzi la  Wananchi wa Tanzania (JWTZ)  Kanali Wilbert  Ibuge akiwasilisha mada katika mafunzo hayo amesema kuwa  Tanzania ni miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa Barani Afrika zilizotoa mchango mkubwa na kuratibu kuanzishwa kwa mtangamano wa  SADC.

“Hadi sasa hali ya amani na usalama imeendelea kuimarika katika SADC kama inavyojidhihirisha kwa takribani nchi zote za SADC  ambapo nchi wanachama ziliazimia kusimamia maendeleo ya kiuchumi ya Kanda kwa kuzingatia malengo ikiwemo kukuza uchumi, kuondoa umasikini, kuboresha hali ya maisha ya wananchi.

Msingi wa SADC ni kusimamia malengo yake ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii sambamba na yale ya ulinzi na usalama unabainishwa katika Ibara ya 2 ya mkataba wa SADC ( Article 2 of SADC Treaty).


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527