SAUTI INAYODAIWA KUWA NI YA KINANA, NAPE YAMUIBUA LUSINDE.....ALITAKA JESHI LA POLISI LIWAHOJI


Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola ameombwa kuliagiza Jeshi la Polisi kumhoji Nape Nnauye na Abdulrahman Kinana kwa madai kuwa wamemtukana Rais John Magufuli.


Ombi hilo limetolewa na Mbunge wa Mtera (CCM), Livingstone leo katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaaam.


Mbali na hilo, Lusinde amesema ndani ya CCM hakuna mgogoro isipokuwa kuna watu  wachache wanaoulumbana na mtu mmoja mmiliki magazeti nchini,  jambo ambalo haliwezi kuitwa mgogoro ndani ya chama hicho..

”Nataka niseme kuwa wazee wangu wamepotoka kwa kutoa waraka  huo; walitakiwa wamtafute kijana wa kumjibu Musiba, au wao wenyewe watafute press (mkutano wa habari) wamjibu Musiba siyo kuandika waraka utakaobaki maishani mwao kwamba viongozi wa kisiasa wa ngazi za juu,  Kinana na Makamba,  waliuandika kumlalamikia Musiba, vitu ambavyo naona vimewafedhehesha sana.” alisema Lusinde.

Kuhusu sauti  zinazodaiwa kuwa ni za Kinana na Nape, alisema zina maneno ya fedheha kwa viongozi wa nchi hii, na ndiyo maana akamtaka Lugola awaite Kinana na Nape awahoji kwa kutoa maneno ya kashfa kuhusiana na uongozi wa nchi hii. 


Akigusia msimamo wa aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa awamu ya nne, Bernard Membe, alisema atamshughulikia pindi akirejea kutoka ziara ya kikazi nchini China.


"Kuna mtu mmoja anaitwa Bernard Membe namuona anavyohangaika hangaika leo nina safari ya kwenda China kwa ziara ya kikazi, Membe namuweka kiporo nikirudi nitashughulika nae kwasababu namjua vizuri na hana chochote" Amesema Lusinde


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527