RAIS MAGUFULI AMPIGIA SIMU RAIS UHURU KENYATTA NA KUMSHUKURU KWA DHAHABU ILIYORUDISHWA NCHINI


Rais Magufuli amempigia simu Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta na kumpa ujumbe wa shukrani kwa kuwezesha urudishwaji wa dhahabu kilo 35.34 na fedha zilizoibiwa hapa nchini na kupatikana nchini Kenya.


Rais Magufuli amefanya hivyo leo Jumatano Julai 24, walipozungumza kwa njia ya simu wakati wa makabidhiano ya dhahabu iliyokamatwa nchini Kenya na kuwasilishwa  na Mjumbe Maalum wa Rais Kenyatta yaliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.

“Ninakushukuru sana Mh Rais, Dada yangu Monica ameshashusha mzigo hapa na nimeuona ni wenyewe, fedha na dhahabu hizi tunazokusanya nilikuwa nawaambia Watanzania kama tungekuwa watu wabaya wasingeziona kabisa na ndiyo maana nawaambia Rais Kenyatta ni mzalendo sana na ndiyo sababu tumezitoa hadharani.

“Nataka uwapongeze sana vyombo vya ulinzi na usalama vya Kenya kwasababu hii mali haikushikwa na vyombo vya ulinzi na usalama vya Tanzania, nitatafuta zawadi ya kuwapa kwa niaba ya Watanzania na naomba kama wana mbinu nyingine wanatumia wawafundishe na wenzao wa Tanzania.

“Nashukuru sana ulivyomtuma Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Monica Juma mbali ya kuwa ni mzuri anachapa kazi na anaiwakilisha Kenya vizuri,” amesema Rais Magufuli huku akicheka.

Naye Rais Kenyatta akijibu ujumbe huo amesema wananchi wa Kenya na Tanzania waliwaamini na kuwapatia nafasi ya kuwaongoza hivyo watafanya kila linalowezekana kuilinda imani hiyo.

“Tulisema mali ya wananchi wetu lazima irudi kwa wananchi wetu, wametupatia imani yao na kutupatia uongozi hivyo kazi yetu ni kuhakikisha tunalinda mali zao wetu zikatumike kujenga barabara na shule ili kuunganisha wananchi na walaghai hawana nafasi tena katika nchi zetu,” amesema Rais Kenyatta.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527