Mhe Hasunga Aanza Ziara Ya Ukaguzi Wa Shughuli Za Maendeleo Jimboni Vwawa Mkoani Songwe

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Songwe
Mbunge wa Jimbo la Vwawa Mkoani Songwe ambaye pia ni Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga ameanza ziara ya ukaguzi wa shughuli za maendeleo katika Jimbo la Vwawa.

Akiwa katika kata ya Iyula Mhe Hasunga amekagua ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa na kuzungumza na wanafunzi wa shule ya msingi Iyula ambapo pamoja na mambo mengine amewasisitiza wanafunzi hao kusoma kwa bidii ili kujikwamua katika wimbi la ujinga kadhalika kiuchumi.

Waziri Hasunga amewapongeza walimu wa shule hiyo kwa mshikamano na usimamizi madhubuti wa fedha za ujenzi wa vyumba hivyo viwili vya madarasa ambavyo vimefikia katika hatua nzuri ya kuanza kutumika.

“Mna bahati sana kusoma katika shule ambayo imetoa waziri wa kilimo hivyo ili kuwa na viongozi wengi katika Taifa hili mnapaswa kusoma kwa bidii na kuongeza ufaulu katika Takwimu za mkoa wetu” Alisema Mhe Hasunga

Pamoja na kuchangia shughuli za maendeleo katika jimbo hilo la Vwawa lakini pia amewataka wanafunzi hao kutambua kuwa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli imejipanga kuimarisha elimu na imeanza na utoaji wa elimu bure kuanzia ngazi ya awali mpaka sekondari.

Alisema kuwa lengo la Rais Magufuli kuruhusu elimu kuwa bure ni kutaka kurahisisha upatikanaji wa elimu kwa urahisi kwa wanafunzi wote nchini ili hata wale waliokosa fursa kutokana na kipato duni cha wazazi waweze kuelimika na kuwa msaada katika familia zao na Taifa kwa ujumla.

Mhe Hasunga amesema kuwa pamoja na vitabu kuwasaidia wanafunzi kuelimika lakini wazazi na walimu ni sehemu ya uimara wa mafanikio ya wanafunzi katika ufaulu wao.

“Mimi nawapongeza sana ninyi wanafunzi kwani mna bahati kubwa kusoma katika kata zenu mnazoishi maana sisi wakati tunasoma tulikuwa tukienda umbali mrefu kutafuta elimu jambo ambalo lilikuwa likitukatisha tamaa ya kusoma” Alikaririwa Mhe hasunga

Mbunge wa Jimbo la Vwawa Mkoani Songwe ambaye ni Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga atakuwa na ziara ya siku tano katika jimbo hilo ambapo pamoja na mambo mengine atashirikiana na wananchi katika shughuli za maendeleo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments