SERIKALI YADHAMIRIA KUIMARISHA HUDUMA KWA WATU WENYE ULEMAVU


Na; Mwandishi Wetu
Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na wadau imedhamiria kuboresha huduma na upatikanaji wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu.

Akizungumza wakati wa hafla ya kupokea vifaa saidizi kwa ajili ya watu wenye ulemavu iliyoandaliwa na Kampuni ya Sigara Tanzania (TCC Plc), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama alisema kuwa kundi la Watu wenye Ulemavu lilikosa baadhi ya fursa hapo awali kutokana na changamoto ambazo wamekuwa wakikabiliana nazo.

“Tunafahamu watu wenye ulemavu wanauhitaji wa huduma bora na vifaa saidizi vitakavyo wawezesha kumudu mazingira ili nao waweze kujumuika katika nyanja zote,” alisema Mhagama

Alifafanua kuwa takwimu na Sensa ya Taifa ya Watu wenye na Makazi ya mwaka 2012, imekadiria idadi ya watu Tanzania ni zaidi ya milioni 44 ambapo milioni 2.5 ni Watu wenye Ulemavu.

Waziri Mhagama alisema, Serikali imeazima kuboresha huduma kwa Watu wenye ulemavu ikimemo kutoa elimu bure na kuimarisha elimu jumuishi, kujenga vituo vya afya na hospitali pamoja na utoaji wa matibabu bure kwa watu wenye ulemavu wasio na uwezo.

Mbali na hayo, alihimiza wadau pamoja na makampuni kuona umuhimu wa kuhudumia kundi la watu wenye ulemavu wakiwa wanatoa huduma mbalimbali za kijamii.

Aidha, alipongeza Kampuni ya Singara Tanzania (TCC) kwa msaada huo na kuwashauri waendelee kukumbuka kundi hilo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Sheria na Uhusiano wa TCC, Bw. Godson Killiza alisema kuwa watu wenye ulemavu wana uwezo mkubwa na nijukumu kama wadau kuwasaidia na kuwaunga mkono kwenye masuala mbalimbali.

Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la Watu wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) Bi. Ummy Nderiananga alieleza kuwa juhudi za Serikali katika kushirikiana na wadau itasaidia kwa kiasi kikubwa kuondoa changamoto za Watu wenye Ulemavu katika kufanikisha masuala yao.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527