Picha : MBUNGE AZZA HILAL ATOA MSAADA WA KOMPYUTA SHULE YA SEKONDARI SOLWA

Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) ametoa msaada wa Kompyuta nne zenye thamani ya shilingi milioni 8 katika shule ya Sekondari Solwa iliyopo katika jimbo la Solwa mkoani Shinyanga ili waitumie katika masomo yao kuendana na ulimwengu wa teknolojia.

Kompyuta hizo ni sehemu ya Kompyuta 15 zenye thamani ya shilingi milioni 30 zilizopatikana kutokana na juhudi za Mbunge Azza Hilal Hamad kwa kushirikiana na wadau ambao ni Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwa ajili ya shule mbalimbali mkoani Shinyanga.

Akikabidhi Kompyuta hizo kwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko leo Juni 7,2019 katika shule ya sekondari Solwa,Mhe. Azza amesema kupitia kompyuta hizo wanafunzi watajifunza teknolojia ya kisasa.

“Nimeleta kompyuta hizi 4  aina ya Dell kwenye shule hii ya Solwa yenye jumla ya wanafunzi 708 kwa sababu nataka na nyinyi muijue kompyuta. Nimeona ni vizuri angalau tukaangalia shule zilizopo pembezoni walau wanafunzi wakapata uelewa wa kompyuta angalau kwa uchache wa hizi nilizopata”,alisema Azza.

“Kilichonisukuma ni kuona shule zetu nyingi za vijijini mwanafunzi hadi anamaliza kidato cha nne hata sura ya Computer haijui, kwa hiyo inakuwa changamoto kubwa pale anatoka shuleni na kuendelea na masomo ya kidato cha tano au chuo Computer inaonekana ni kitu kigeni kabisa kwake”,aliongeza.

Mhe. Azza aliushukuru Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwa kushirikiana naye kuhakikisha angalau shule za sekondari mkoani Shinyanga zinapata kompyuta ili watoto waweze kujifunza teknolojia ya kisasa.

“Nawashukuru sana UCSAF kwa kunipatia kompyuta, nitaendelea kuwasumbua naomba msinichoke kwani shule nyingi Shinyanga hazina kompyuta. Niwaombe pia wadau wengine waweze kutusaidia katika mkoa wa Shinyanga ili kuondoa changamoto ya Kompyuta katika shule zetu”,alisema Azza.

Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko alimshukuru mbunge huyo kwa kufanikisha kupatikana kwa kompyuta hizo na kuwataka wanafunzi kutunza na kuzitumia vizuri katika kujifunzia masomo yao.

“Sasa hivi dunia imebadilika imekuwa ya Kidigitali zaidi,tumieni kompyuta hizi kujifunza mambo mazuri,mbali na kujifunzia masomo mnaweza kuzitumia pia kupata taarifa mbalimbali za nchi hii. Nanyi walimu hakikisheni mnawasimamia vizuri wanafunzi hawa”,alisema Mhe. Mboneko.

Naye Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Mhe. Hoja Mahiba alisema shule ya sekondari Solwa imekuwa ya kwanza kwenye halmashauri hiyo kupata kompyuta kupitia mbunge Azza na kubainisha kuwa zitasaidia kuwaandaa wanafunzi katika maisha yao.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (wa pili kulia) na Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko (wa tatu kushoto) wakipokelewa na viongozi mbalimbali wa kata ya Solwa wakati wakiwasili katika shule ya sekondari Solwa kwa ajili ya zoezi la makabidhiano ya Kompyuta leo Juni 7,2019.wa pili kushoto ni diwani wa kata ya Solwa Mhe. Awadhi Aboud.Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) akizungumza wakati wa kukabidhi kompyuta nne kwa ajili ya wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa leo.Kushoto  Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Mhe. Hoja Mahiba. Kulia ni Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza katika shule ya sekondari Solwa wakati akipokea kompyuta zilizopatikana kwa juhudi za mbunge Azza Hilal.
Wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa wakimsikiliza Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko.
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) akikabidhi moja ya kompyuta hizo aina ya Dell kwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko (kulia) kwa ajili ya wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa.
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) akishikana mkono na Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko (kulia) wakati wa makabidhiano ya kompyuta hizo kwa ajili ya wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa.
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad (CCM) na  Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko (kulia) wakifurahia wakati wa kukabidhiana Baobonya ya kompyuta.
Wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa wakiwa wamebeba moja ya kompyuta zilizotolewa na Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad.
Wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa wakiwa wamekaa wakati wa makabidhiano ya kompyuta.
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad akiwasisitiza wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa kuzingatia masomo yao na kuacha tamaa ya mapenzi ili waweze kutimiza ndoto zao.
Kaimu Afisa Elimu halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Jesse George akimshukuru Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad kwa kuwapatia kompyuta ambazo zitawasaidia wanafunzi katika masomo na maisha yao.
Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Mhe. Hoja Mahiba akizungumza wakati wa makabidhiano ya kompyuta huku akiwataka wanafunzi wa kike kutoa taarifa kwa walimu na viongozi mbalimbali pale wanaume wenye tamaa za mapenzi wanapowasumbua.
Mkuu wa shule ya sekondari Solwa ,Paul Kakome akimshukuru Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad kwa kuwapatia msaada wa kompyuta.
Diwani wa kata ya Solwa Mhe. Awadhi Aboud akimshukuru Mbunge Azza Hilal kwa msaada wa kompyuta kwa wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa huku akielezea misaada mbalimbali ambayo imekuwa ikitolewa na Mbunge huyo kwa ajili ya maendeleo ya wananchi katika sekta ya elimu na afya.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko akiwasisitiza wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa kuepuka mimba na ndoa za utotoni.
Kushoto  Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Mhe. Hoja Mahiba akifuatiwa na Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad na Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko wakifurahia jambo wakati wa makabidhiano ya kompyuta kwa ajili ya wanafunzi wa shule ya sekondari Solwa.
Mbunge wa viti Maalum Mkoa wa Shinyanga Mhe. Azza Hilal Hamad  akiagana na wanafunzi wa shule ya Sekondari Solwa baada ya kuwakabidhi kompyuta nne aina ya Dell ili wazitumie kujifunzia masomo yao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527