SHULE YA VIZIWI BUGURUNI KUSHIRIKI LIGI YA MPIRA WA MIGUU


Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Buguruni ya viziwi ,Milembe Kulwa akipokea vifaa michezo kutoka kwa Meneja Masoko wa X-TIGI,Said Adinan vyenye thamani ya zaidi ya laki tatu leo jijini Dar es Salaam.(Picha na Emmanuel Massaka wa Michuzi Tv)
Wanafunzi wa shule ya msingi Viziwi Buguruni wakionesha Vipaji vyao vya kucheza mpira.
Picha ya pamoja.

Yapewa vifaa vya michezo vya zaidi ya shilingi laki tatu

Na Leandra Gabriel, Blogu ya jamii

SHULE ya msingi ya watu wenye mahitaji maalumu Buguruni viziwi inataraji kushiriki mashindano ya michezo ya wanafunzi wenye mahitaji maalumu yanayoshirikisha shule za jiji la Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari Afisa elimu Manispaa ya Ilala Elizabeth Thomas amesema kuwa wamejiandaa kutetea vikombe vyote katika ligi hiyo kwa watu wenye mahitaji maalumu, amesema kuwa wataingia kambini kwa siku 10 ili kupata timu ya Wilaya.

Amesema kuwa changamoto kubwa kwa sasa ni upungufu wa jezi, mipira pamoja na viatu na amewaomba wadau mbalimbali kujitokokeza na kuwasaidia watoto hao.

Kwa upande wake mkuu wa shule ya msingi Buguruni viziwi Mirembe Kurwa ameshukuru kwa msaada huo na kuahidi ushindi kwa Manispaa ya Ilala, na kusema kuwa wataendelea kushiriki michezo kupitia UMITASHUMTA kila mwaka.

Pia amesema kuwa watoto wenye ulemavu ni sawa na watoto wengine hivyo hatuna budi kuwalinda na kutetea haki zao pamoja na kuwafanya wajisikie kama watoto wengine.

Kwa upande wake meneja masoko Said Adinan kutoka X-TIGI mobile amesema kuwa wametoa zawadi chache ili kuweza kuwasaidia na kuwainua vijana hao kimichezo na kuwataka wadau wengine kuwaangalia watoto wenye mahitaji ya aina hiyo.

Adinan amesema kuwa wao kama ofisi wataangalia namna ya kuwasaidia watoto hao kwa kuanza na mshindi atakayeibuka katika mashindano hayo.

Mashindano hayo ya watoto wenye mahitaji maalumu yatashirikisha shule zote zenye mahitaji maalumu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post