MWANZILISHI WA WIKLEAKS AKAMATWA UINGEREZA


Muasisi wa mtandao wa WikiLeaks, Julian Assange, leo ametolewa kwa nguvu kutoka ubalozi wa Ecuador jijini London na kutiwa kwenye karandiga ya polisi ya Uingereza.

Polisi wa Uingereza wamemtia mbaroni Assange kutokana na waranti wa mahakama wa tangu mwaka wa 2012, baada ya Ecuador, taifa la Amerika Kusini, kuamua kufuta kibali cha uhamiaji kutokana na sababu za kisiasa, ambacho kilimpa Assange ulinzi wa kutokamatwa kwa kipindi cha karibu miaka saba. 

Katika taarifa polisi imesema Assange anazuiliwa katika kituo kimoja cha polisi katikati mwa London mpaka atakapopandishwa kizimbani katika mahakama ya Westminster haraka itakavyowezekana.


Rais Lenín Moreno wa Ecuador alisema kupitia mtandao wa Twitter kuwa nchi yake imechukua uamuzi wa kusitisha hali ya hifadhi ambayo ilimpa Assange baada ya “ukiukwaji wake wa mara kwa mara wa taratibu kwenye mikutano ya kimataifa na taratibu za maisha ya kila siku, uamuzi ambao uliwapa nafasi Mamlaka ya Uingereza kumkamata.

Idara ya Haki ya Umoja wa Mataifa imetoa mashtaka ya jinai dhidi ya Assange, mwenye umri wa miaka 47, kuhusiana na kuchapishwa kwa nyaraka zilizowekwa rasmi, ukweli ambao waendesha mashtaka waliuweka wazi kwa umma mwezi Novemba.

Assange ambaye ni raia wa Australia na mtaalamu wa masuala ya kutengeneza programu za computer amepata hifadhi katika jengo la Ubalozi wa Euador, London Uingereza tangu 2012 na amekuwa akitafutwa na Serikali ya Marekani kwa mashitaka ya kuvujisha siri za serikali kupitia mtandao wake wa Wikileaks.

Aidha kutokana na mikataba ya kimataifa kuhusu masuala ya kidiplomasia serikali ya Uingereza ilikuwa haiwezi kumkamata Assange akiwa ndani ya ubalozi wa Ecuador kwani ubalozi huo unahesabiwa kama ni ardhi ya nchi hiyo ya Amerika ya Kusini.

Wikileaks ilikuwa inaweka wazi mawasiliano ya kikazi ya Clinton aliyokuwa akifanya kupitia barua pepe za msaidizi wake binafsi badala ya kutumia zile za kiserikali, na Trump, wakati wa kampeni, alikuwa anayataja sana mapungufu ya mshindani wake huyo wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje chini ya utawala Barack Obama.

Kwa mfano Machi mwaka juzi mtandao wa Wikileaks ulisambaza habari kuhusu namna Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) lilivyokuwa linafanya udukuzi wa mitandao ya watu wengine, habari ambazo utawala wa Trump haukupenda watu wengine wajue.

Assange aliuanzisha mtandao wa Wikileaks mwaka 2006 ambapo ulianza kuchapisha milolongo ya uvujaji wa habari za siri alizopatiwa na askari mmoja wa Marekani Chelsea Manning aliyeziiba.

Awali habari nyingi za uvujaji zilihusu vita ya Afghanistan na ile ya Iraq. Baada ya uvujaji wa mwaka 2010 serikali ya Marekani ilianza uchunguzi kuhusu Wikileaks hususan nani mhusika na kuomba mataifa mengine rafiki kusaidia.

Desemba 7 2010 Assange alijisalimisha kwa mamlaka za kipolisi za Uingereza na alishikiliwa kwa siku 10 na baadaye kuachiwa kwa dhamana. Baadaye aliomba na kukubaliwa rasmi hifadhi katika ubalozi wa Ecuador Agosti 2012.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527