KIMBUNGA KENNETH CHABADILI UELEKEO


Mamlaka  ya Hali ya Hewa (TMA), imewataka wananchi wa mikoa ya Mtwara na Lindi kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwa sababu kimbunga ambacho kilitarajiwa kusababisha athari kwenye ukanda huo kimebadili mwelekeo.


Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk. Agnes Kijazi, alitoa kauli hiyo jana na kueleza kuwa kimbunga hicho kimekwenda kusini zaidi mwa Pwani ya Msumbiji, lakini akatahadharisha kuwa bado kipo kwa kuwa kitarudi tena baharini.

"Kwa sasa, kimbunga bado kipo ardhi ya Msumbiji na mwishoni mwa wiki kinatarajia kurudi baharini kama tulivyoeleza awali kwa kitaalamu, tunaomba wananchi kwa sasa waendelee na shughuli zao huku wakiendelea kufuatilia utabiri wa TMA,” alisema.

Dk. Kijazi alisema kimbunga hicho kitakaporejea baharini kama walivyoeleza awali, kitaleta athari ukanda huo wa kusini lakini wananchi wataarifiwa ili wachukue tahadhari.

Alisema kwa wakati huo aliokuwa anazungumza, hali ya hewa ya mikoa ya Lindi na Mtwara ilikuwa ya mawingu ambayo hayakuwa na athari.

“Maeneo ya Magharibi mwa Ziwa Viktoria kuna wingu zito limetanda. Tunawapongeza sana wananchi kwa kusali na kutii kwa kwenda maeneo maalum yaliyotengwa huku wasipate athari. Tunazishukuru mamlaka mbalimbali, zimeonyesha ushirikiano mkubwa kwenye suala hili," alisema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527