KESI YA ZITTO KABWE YAKWAMA TENA


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imepanga kusikiliza kwa siku mbili mfululizo kesi ya Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Zuberi Kabwe.

Kesi hiyo ya 'uchochezi' ya Jinai Na. 327 ya Mwaka 2018, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu aleo iliitwa kwa ajili ya kusikiliza ushahidi wa upande wa mashtaka, ambapo imeahirishwa hadi tarehe 24 na 25 Aprili 2019.

Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Huruma Shaidi kutokana na upande wa mashtaka kwa mara nyingine kushindwa kumleta mahakamani shahidi wao kwa madai kwamba shahidi huyo yupo kwenye operesheni maalum ya Jeshi la Polisi.

Mawakili wa utetezi Wakili Peter Kibatala na Wakili Stephen Mwakibolwa hawakuwa na pingamizi kwa maombi ya shauri hilo kupangiwa tarehe nyingine.

Hakimu Huruma Shaidi amesema kwamba amepanga kusikiliza ushahidi wa kesi hiyo kwa siku mbili mfululizo ili imalizike kwa muda uliopangwa hivyo upande wa mashtaka uhakikishe unaleta mashahidi wake wake kwenye muda uliopangwa.

Inadaiwa kuwa Oktoba 28,2018 katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika ofisi za makao makuu ya Chama cha ACT Wazalendo, kiongozi huyo alitumia maneno yenye kuleta kuleta chuki miongoni mwa wananchi wa Tanzania dhidi ya Jeshi la Polisi.

Mbunge huyo alifikishwa Mahakama ya Kisutu kwa mara ya  kwanza, Novemba 2, 2018, kwa sasa bado Zitto anaendelea na dhamana.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527