CREDIT SUISSE BANK: TUTAENDELEA KUIKOPESHA TANZANIA KWA KUWA INAKOPESHEKA NA MAHIRI KATIKA USIMAMIZI WA MIRADI

Na Benny Mwaipaja, WFM, Washington DC

Benki ya Credit Suisse ya Uingereza imeahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuikopesha Tanzania ili kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo baada kuridhishwa na uaminifu wa urejeshaji mikopo kwa wakati pamoja na ubora wa viwango vya miradi inayotekelezwa nchini.

Ahadi hiyo imetolewa Mjini Washington D.C nchini Marekani na Mkurugenzi wa Masoko ya Kimataifa wa Benki hiyo Bi. Elizabeth Muchemi, alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, katika mikutano ya kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha na Kimataifa inayoendelea Mjini, Washington D.C.

Bi. Elizabeth Muchemi amesema uzoefu unaonesha kuwa baadhi ya nchi zinazochukua mikopo hazitekelezi ipasavyo miradi iliyoombewa fedha jambo ambalo ni tofauti kwa Tanzania ambayo miradi iliyoombewa mkopo inatekelezwa vizuri na kwa viwango.

Hivi karibuni benki hiyo iliikopesha Tanzania mkopo wa dola za Marekani milioni 200 kwa ajili ya kutekeleza miradi mabalimbali ya maendeleo ikiwemo sekta miundombinu ya barabara na reli.

“Tuko tayari kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania kwa kadri Serikali itakavyoona kwa sababu ya mipango mizuri ya Serikali pamoja na kulipa madeni kwa wakati. Benki ya Credit Suisse haijawahi kuwa na tatizo na Tanzania katika urejeshaji wa mikopo jambo linaloongeza imani kwa Tanzania” alisema Bi. Elizabth Muchemi.

Akizungumza na Mwakilishi huyo wa Benki ya Credit Suisse katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani, katika kikao kilichohudhuriwa pia na Gavana wa Benki Kuu Prof. Florens Luoga, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango ameishukuru Benki hiyo kwa utayari wake wa kuendelee kushirikiana na Serikali katika ugharamiaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Amesema kuwa Taifa limejipanga kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo reli, barabara, umeme, maji, elimu, afya,  mradi wa gesi kimiminika (LNG), usafiri wa anga na majini, bandari, elimu, ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda hadi Tanzania, mradi ambayo inahitaji uwekezaji mkubwa   wa rasilimali fedha.

Dkt. Mpango amesema Tanzania inataka kutumia uwepo wa nchi zisizopakana na bahari kama vile Burundi, Uganda, Rwanda, na Jamhuri ya Congo kujenga mtandao wa reli ya kisasa na barabara utakao saidia kuchochea biashara na kukuza uchumi wa nchi na ukanda huo kwa ujumla.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527