KIGOGO WA TAKUKURU ANAYEDAIWA KUWADHULUMU WENZAKE VIWANJA, KULTHUM MANSOOR AMEKAMATWA

Mkurugenzi wa Mipango TAKUKURU Kulthum Mansoor, ambaye jana Machi 28, 2019, alitajwa na Rais Magufuli kwa tuhuma za kuwadhulumu viwanja, baadhi ya wafanyakazi wenzake wa TAKUKURU amekamatwa na kufikishwa kituo cha Polisi Oysterbay.


Kwa mujibu wa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali John Mbungo,  Kulthum alikamatwa jana Alhamisi Machi 28, 2019 na kupelekwa kituo cha polisi cha Oysterbay, jijini Dar es Salaam ambapo leo Ijumaa March 29 atafikishwa mahakamani.



Jana, Rais Magufuli akizungumza Ikulu mara baada ya kumuapisha Balozi wa Tanzania nchini Cuba, Valentino Mlowola alisema kuna mkurugenzi mmoja wa makao makuu Takukuru aliwauzia viwanja hewa wafanyakazi wenzake, lakini anashangaa hajapelekwa mahakamani hadi sasa.

“Wala sijapata taarifa kwamba hizo fedha amezirudisha kwa wafanyakazi aliowadhulumu. Wafanyakazi wanaumia, wanalalamika pembeni.

“Amewadanganya kwamba ana viwanja Bagamoyo, lakini mpaka leo hawajapewa,” alisema Rais Magufuli.

Alisema kashfa hiyo iliibuliwa tangu Balozi Mlowola alipokuwa mkurugenzi wa taasisi hiyo, lakini hadi sasa hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.

“Suala hili lilianza tangu wakati wa Balozi Valentino, nikamuuliza huyu mbona harudishi fedha au hapelekwi mahakamani, akawa na kigugumizi, sasa na wewe usiwe na kigugumizi kwa sababu nafasi za ubalozi zimeisha.

 “Ndiyo maana huwa najiuliza hawa Takukuru huwa ni kwa ajili ya watu wengine, wao ‘hawaji-takukuru’ humo humo ndani?” alihoji.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527