MWANAMKE AUAWA KWA KUTAFUNWA NA NGURUWE

Mwanamke mmoja nchini Urusi ameuawa na nguruwe aliokuwa anawafuga baada ya kuanguka kwenye banda la wanyama hao.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Urusi, mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 56 alikuwa akiwalisha nguruwe ndipo ghafla akaanguka na nguruwe hao wakamtafuna.

Inasadikiwa kuwa chanzo cha kuanguka kwake ilikuwa ni kuzirai ama kupatwa na kifafa.

Tukio hilo limeripotiwa kwenye wilaya Malopurginsky jimboni Udmurtia, lililopo katikati ya Urusi.

Vyombo vya habari vya Urusi vinaarifu kuwa mume wa marehemu alikuwa amelala wakati mkewe alipokuwa akiwahudumia nguruwe hao. Bwana huyo inasemekana alikuwa mgonjwa.

Baada ya kuamka alianza kumtafuta mkewe na kukuta mwili wake ndani ya banda la nguruwe.

Inataarifiwa kuwa alifariki baada ya kupoteza damu nyingi. Tayari upelelezi wa polisi juu ya tukio hilo umeshafunguliwa. 

Oktoba mwaka 2012 tukio kama hilo liliripoptiwa nchini Marekani katika jimbo la Oregon. Bwana Terry Vance Garner, aliyekuwa na miaka 69 wakati huo alienda kuwalisha nguruwe wake lakini hakurejea.

Baadae, familia yake ilikuta mabaki ya mwili wake kwenye banda la nguruwe huku sehemu kubwa ya mwili huo ikiwa imeshaliwa na wanyama hao.

Mamlaka za eneo hilo ziliripoti kuwa mmoja wa nguruwe hao hapo awali alishawahi kumng'ata marehemu lakini aliweza kujinasua.

Kaka wa bwana huyo, Michael, alidai kuwa nguruwe hao walishawahi kujaribu kumtafuna na yeye na bwana Garner aliahidi kuliua dume kubwa ambalo ndio lilikuwa tishio zaidi.

Hata hivyo, baadae alibadili mawazo na kuendelea kuwafuga mpaka pale walipomuua.
Chanzo- BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527