LUGOLA " KAULI YA KUINGIA POLISI NI BURE NA KUTOKA NI HELA NATAKA NIIFUTE'

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kangi Lugola amesema ataendelea kufanya ziara za kushtukiza katika vituo vya polisi mbalimbali nchini ili kubaini kama maagizo yanayotolewa na serikali yanatekelezwa.

Lugola amesema hayo leo Jumanne Novemba 20, alipofanya ziara ya kushtukiza katika Kituo cha Polisi Chang’ombe jijini Dar es Salaam ambapo amefanya ukaguzi na kuzungumza na mahabusu waliopo kituoni hapo.

Pamoja na mambo mengine, Lugola amemuagiza mkuu wa kituo hicho kwa kushirikiana na polisi kufanya operesheni maalumu ya kuyapitia majalada yote na kuangalia mahabusu ambao kesi zao ziko tayari kwenda mahakamani wapelekwe na wenye kesi zinazodhaminika pia wapatiwe dhamana.

“Kuna watu wamekaa humu muda mrefu na ukiulizia kesi yake unaona inadhaminika kabisa ila wapo tu ndani ufanyike utaratibu watu hawa waondolewe na tubaki na ambao ni lazima tuwashikilie wakati wakisubiria miendendo ya kesi zao.

Aidha lugola ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi kwa kuwafichua wahalifu ila wasiwasingizie kesi kwa sababu ya maslahi yao binafsi.

“Kuna Watanzania wanawatumia polisi wachache wasio wazalendo kuwabambikia kesi watu wasio na hatia wanawekwa ndani muda mrefu ndugu zao wakifuatilia wanaambiwa watoe fedha ndiyo mtu wao atoke, hii kauli ya kuingia polisi ni bure na kutoka ni hela nataka niifute,” amesisitiza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527