DIWANI WA CHADEMA 'ALIYEPIGWA STOP' KUINGIA KWENYE VIKAO KUTINGA MAHAKAMANI...ADAI MKURUGENZI ANATUMIA MADARAKA VIBAYA


Diwani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kata ya Ngokolo manispaa ya Shinyanga Emmanuel Ntobi, anatarajia kwenda Mahakamani kupinga maamuzi ya kusimamishwa kuhudhuria vikao vitatu vya baraza la madiwani la manispaa hiyo, kwa kumtuhumu mkurugenzi Geofrey Mwangulumbi kujimilikisha viwanja vinane kinyume na taratibu.


Amebainisha hayo leo Novemba 2, 2018 wakati akizungumza na vyombo vya habari mjini Shinyanga kwenye ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Katemi, ambapo amesema kuwa hajaridhika na maamuzi hayo ya kusimamishwa kwake, ambapo hivi karibuni anatarajia kwenda mahakamani na jopo la wanasheria watano, ili kupinga maamuzi hayo ambayo ni batiri yaliyolenga kuhalalisha ufisadi ndani ya halmashauri hiyo.


Amesema kanuni iliyotumika kumsimamisha kuhudhuria vikao vya baraza hilo imekiukwa, ambapo yeye alitoa kama mawazo huru kwenye baraza kuwa, Mkurugenzi anatumia madaraka yake vibaya kujimilikisha viwanja, kama kanuni ya 27 ya mwaka 2013 ya halmashauri inayosema, ambapo ilipaswa kuundwa tume huru ili kumchunguza.

“Kwa mujibu wa kanuni ya 27 ya kudumu ya halmashauri ya manispaa ya mwaka 2013, mimi kama mjumbe wa baraza, nina haki ya kutoa mawazo yangu huru ndani ya baraza na yakafanyiwa kazi, na kama nilionekana kutoa kashifa basi meya angeniambia nitengue kauli yangu ndani ya baraza na siyo kuanza kuhojiwa nje,”amesema Ntobi.

“Hakuna Sheria wala kanuni inayosema mjumbe akitoa hoja ndani ya baraza aitwe kuhojiwa nje, ambapo kama mimi nilionekana kutoa kashfa, ningeambiwa nitengue kauli pamoja na kuandika barua ya kuomba radhi ndani ya siku Saba, na siyo kama ilivyotumika kunisimamisha huo ni uonevu tu,”ameongeza.

Pia amesema kutokana na misimamo yake ndani ya baraza hilo kuibua madudu na ufisadi wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa matumizi mabaya ya fedha, ndio zimekuwa zikipangwa njama za kumkandamiza ili kumziba mdomo, ikiwemo na kumsimamisha kutohudhuria vikao ili wapitishe mambo yao.

Aidha katika baraza la madiwani la manispaa ya Shinyanga la kawaida la Oktoba 30, 2018, akisoma taarifa ya kamati ya maadili Naibu Meya wa manispaa hiyo John Kisandu, alisema diwani huyo amesimamishwa kutohudhuria vikao vitatu na kukosa stahiki zake zote, kutokana na kukataa kudhibitisha kauli yake pamoja na kuto omba msamaha kwa maandishi.

Na Marco Maduhu - Malunde1 blog

TAZAMA PICHA HAPA CHINI
Diwani wa Chadema Kata ya Ngokolo Emmanuel Ntobi akizungumza na waandishi wa habari kupinga maamuzi ya kisimamishwa vikao vitatu vya baraza la madiwani, huku akionyesha nyaraka mbalimbali za madudu yanayofanywa na manispaa hiyo ya matumizi mabaya ya fedha za miradi ya maendeleo ikiwamo ya ufadhili ya Word Bank likiwamo Chinjio la mifugo .
Diwani wa Chadema Kata ya Ngokolo manispaa ya Shinyanga Emmanuel Ntobi, akizungumza na waandishi wa habari kupinga juu ya kusimamishwa kwake, na kumtaka waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi Wiliamu Lukuvi kutuma tume ya kuchunguza juu ya ufisadi unaofanywa na manispaa ya Shinyanga kwenye upimaji wa viwanja 30,000.
Kareny Masasy mkono wa kulia ni mwandishi wa gazeti la Serikali (habari leo) akiwa na Suzy Butondo Mwandishi wa Gazeti la Mwananchi wakiwa kwenye mkutano wa diwani wa Chadema  kata ya Ngokolo mnaispa ya Shinyanga Emmanuel Ntobi kupinga maamuzi ya kusimamishwa kutohudhuria vikao vitatu vya baraza.
Waandishi wa habari wakiendelea kuchukua taarifa, kwa diwani wa Chadema Kata ya Ngokolo manispaa ya Shinyanga Emmanuel Ntobi kupinga maamuzi ya kusimamishwa kutohudhulia vikao vitatu vya baraza la madiwani.

Waandishi wa habari wakiendelea kuchua taarifa.

Waandishi wa habari wakichukua taarifa kwenye kikao cha Diwani wa Kata ya Ngokolo Emmanuel Ntobi, wakwanza kushoto ni Velena Kailembo mwandishi wa gazeti la Dira Mtanzania, Katikati ni Stella Ibengwe wa Mwananchi, akifuatiwa na Suleiman Shaghata Mwandishi wa Dailynews.

Waandishi wa habari wakimsikiliza kwa makini diwani wa Kata ya Ngokolo Emmanuel Ntobi kwenye mkutano wake wa kupinga maamuzi ya kusimamishwa kutohudhuria vikao vitatu vya baraza la madiwani, kwa kumtuhumu mkurugenzi wa manispaa hiyo Geofley Mwangulumbi kujimilikisha viwanja Vinane kinyume na taratibu.

Na Marco Maduhu- Malunde 1 Blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527