TANZANIA KUSHIRIKI MAZOEZI YA KIKOSI CHA DHARURA CHA ULINZI WA AMANI CHA SADC NCHINI MALAWI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) zimejipanga kuzuia na kudhibiti madhara yanayosababishwa na machafuko ya kisiasa katika jumuiya hiyo na Bara la Afrika kwa ujumla. 

Wawakilishi wa nchi hizo wamekusanyika nchini Malawi kuanzia tarehe 1 Oktoba hadi 17 Oktoba 2018 kwa ajili ya kufanya mazoezi ya namna ya kutuliza ghasia pamoja na kutoa misaada ya kibinadamu kwa waathirika katika kipindi cha machafuko

Wawakilishi wa Tanzania kutoka Jeshi la Wananchi, Magereza na taasisi za kiraia ikiwemo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ni miongoni mwa watu 600 wanaoshiriki zoezi hilo lililopewa jina la EX UMODZI CPX 2018 na kaulimbiu ya Afrika ni Amani na Maendeleo (Africa for peace and prosperity).

Katika hafla ya ufunguzi wa mazoezi hayo iliyofanyika leo tarehe 08 Oktoba, 2018 katika Chuo cha Kijeshi cha Malawi kilichopo mji wa Salima takriban kilomita 120 kutoka Lilongwe, Naibu Waziri wa Ulinzi wa Malawi, Mhe. Evaton Chemulirenji alisema mazoezi hayo ni utekelezaji wa maazimio ya SADC na Umoja wa Afrika (AU) wa kuandaa kikosi cha kukabiliana na machafuko barani Afrika (Standby Force-SF) ambacho kinatakiwa kiwe kimekamilika ifikapo Januari 2019.

Alisema madhumuni ya mazoezi hayo ni kuhakikisha kuwa kikosi cha SF kinapewa mafunzo ya vitendo ya kutosha ili kiwe na ujuzi na mbinu za kushiriki operesheni za kulinda amani na/au kuingilia kati na kuzuia machafuko (peace keeping and enforcement) pale yanapotokea barani Afrika. Aidha, alisema mazoezi hayo ni muhimu kwa kuwa yatasaidia kuimarisha ushirikiano na kuaminiana baina ya nchi wanachama wa SADC.

Mazoezi hayo yanajumuisha makundi mbalimbali ikiwa ni pamoja na majeshi  ya ulinzi,  askari polisi, askari magereza na raia wa fani tofauti kama vile za Utawala wa Sheria, siasa, mawasiliano, Utawala, haki za binadamu na jinsia ambao wana mchango mkubwa katila masuala ya operesheni za kulinda amani.

Wanajeshi watafanya zoezi la namna ya kutuliza machafuko na raia watajifunza namna ya kusaidia jamii punde tu machafuko yanapodhibitiwa na vikosi vya usalama.
 
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Afrika Mashariki,
Salima,Malawi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527