KAMPUNI YA SUKARI KILOMBERO SASA KUUZA PAKETI NDOGO ZA SUKARI BEI NAFUU


Mkurugenzi wa Biashara wa kampuni ya sukari ya Kilombero Sugar, Fimbo Butallah akizungumza na wananchi wa Mbagala siku ya uzinduzi wa paketi ndogo za sukari ya 'Bwana Sukari' inayozalishwa na kiwanda hicho. Paketi hizo zitauzwa kwa shillingi 500/- na shilingi 1000/-.
Mkurugenzi wa Biashara wa kampuni ya sukari ya Kilombero Sugar, Fimbo Butallah akimkabidhi paketi mpya za Bwana Sukari mkazi wa Mbagala Zena Athumani siku ya uzinduzi wa bidhaa hiyo uliofanyika viwanja vya Mabagala Zakeem hivi karibuni.
Mkurugenzi wa Biashara wa kampuni ya Sukari ya Kilombero Sugar, Fimbo Butallah akizungumza na waandishi wa habari siku ya uzinduzi wa paketi ndogo za sukari ya Bwana Sukari itakayouzwa kwa shillings 500/- and shillingi 1000/-.

***

Kampuni ya Sukari ya Kilombero (KSC) imezindua paketi ndogo za sukari yake ijulikanayo kama ‘Bwana Sukari’, ikiwa ni jitihada za kuhakikisha watanzania wengi zaidi wanamudu kununua sukari hiyo kutokana na unafuu wake wa bei.

Paketi mpya za sukari chapa ya ‘Bwana Sukari’ zinapatikana kwa ujazo wa gramu 350 maarufu kama ‘Robo Plus’ na paketi za gramu 160 maarufu kama ‘Booster’. 

Paketi za ‘Robo Plus’ zitauzwa shilingi 1,000/ kwa kila paketi, na paketi za ‘Booster’ zitauzwa kwa shilingi 500/-kwa kila paketi.

Uzinduzi wa paketi mpya za ‘Bwana Sukari’ uliofanyika maeneo ya Mbagala jijini Dar es Salaam ni sehemu ya mkakati wa kampuni ya KSC kuhakikisha sukari yake inawafikia watanzania wa hali mbalimbali za kiuchumi. Uzinduzi huo ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka Bodi ya Sukari Tanzania (SBT), Chama cha Wazalishaji wa Sukari Tanzania (TSPA), viongozi na wafanyakazi wa KSC.

Akiongea wakati wa hafla ya uzinduzi, Mkurugenzi wa Biashara wa KSC, Fimbo Butallah alisema kampuni ya sukari ya Kilombero imekua ikipanga mikakati ya kuhakikisha bidhaa ya ‘Bwana Sukari’ inawafikia watanzania wengi zaidi hapa nchini.

“Sukari ni moja ya bidhaa muhimu kwa matumizi ya kila siku ya nyumbani na sukari ya Bwana Sukari ni moja ya sukari inayopendwa zaidi na watumiaji wengi, tunawashukuru wateja wetu kwa kuikubali bidhaa yetu na kuifanya ifanye vizuri sokoni, kuonyesha shukrani zetu tumeamua kuwaletea paketi hizi ndogo ili wateja wetu wawe na uhuru wa kuchagua ujazo upi utawafaa kwa matumizi yao,” alisema Fimbo.

Akiongeza kuwa, paketi mpya za ‘Bwana Sukari’ zitakidhi mahitaji ya watumiaji wengi zaidi, “kwa mfano paketi za ‘Booster’ ambazo zitauzwa kwa shilingi 500/-zitawafaa zaidi wale wanaohitaji sukari lakini kwa wakati huo hawana uwezo wa kumudu kununua paketi kubwa au kwa wale wenye familia ndogo.”

“Kwa ufupi, kupitia paketi hizi ndogo za Bwana Sukari tunawapa wateja wetu uhuru wa kununua sukari ya ujazo mdogo lakini iliyofungwa kwa hali ya usafi na usalama kabisa na kwa bei nafuu.”

Kwa kuanzia, paketi mpya za ‘Bwana Sukari ’zitapatikana katika maduka yote ya rejareja mkoani Dar es Salaam na wilayani Kilombero mkoani Morogoro wakati KSC inaendelea kufanya mikakati kuhakikisha bidhaa hii inasambaa nchini kote siku za usoni.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527