HOSPITALI ZA WILAYA 67 KUJENGWA MWAKA HUU WA FEDHA


 Sehemu ya Vifaa vya Kisasa vya Upasuaji kama vinavyoonekana katika moja ya vituo vya afya vilivyojengwa na Serikali ya Awamu ya Tano.

Wataalamu wa afya wakikagua sehemu ya vifaa tiba vipya  katika moja ya Kituo cha afya kilichojengwa na Serikali ya Awamu ya Tano.
(Picha zote na OR- TAMISEMI).


Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma.
SERIKALI ya Awamu ya Tano Kujenga Hospitali za Wilaya 67 katika mwaka huu wa  fedha ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuimarisha sekta ya Afya nchini.

Akizungumza Katika Kipindi cha TUNATEKELEZA Kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na kuratibiwa na Idara ya Habari MAELEZO, Waziri wa Nchi Ofisi  ya Rais TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo amesema kuwa Serikali itatumia shilingi bilioni 105 kutekeleza mradi huo.

 “Tangu tupate uhuru tulikuwa na hospitali za wilaya 77 lakini sasa Serikali ya Awamu ya Tano inaenda kuweka historia kwa mageuzi makubwa yanayofanyika katika sekta hii ya afya na tumejipanga kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata huduma bora za afya,” alisisitiza Mhe. Jafo.

Akifafanua Mhe. Jafo amesema kuwa Serikali  imeweka  historia, kwa kuwa tangu Taifa lipate uhuru kulikuwa na vituo vya afya vinavyofanya upasuaji 115 nchi nzima lakini katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imejenga vituo vya afya vyenye uwezo wa kufanya upasuaji 208 vinavyoenda sambamba na ujenzi wa hospitali za wilaya zinazoanza kujengwa  mwaka huu.

Aidha amesema, Bohari Kuu ya Dawa (MSD) imeshapatiwa fedha ili iweze kusambaza vifaa tiba katika vituo vya afya vilivyojengwa ili viweze kuanza kufanya kazi.

Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Mamlaka za Serikali za Mitaa zimapata mafanikio makubwa katika kuimarisha sekta za elimu,  afya na ujenzi wa miundo mbinu kama barabara, vyumba vya  madarasa na miundo mbinu mingine inayochochea  maendeleo ya wananchi.

Pia ameziagiza Halmashuri zote nchini kusimamia ukusanyaji wa mapato, lengo likiwa ni kuweka mfumo mzuri wa ufuatiliaji ili kuboresha makusanyo na  kusimamia matumizi ya fedha hizo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Nawataka wakurugenzi wote wawe wakali katika ukusanyaji mapato na tutatoa onyo maalum kwa halmashauri zote ambazo hazifanyi vizuri katika ukusanyaji mapato,” alisema Mhe. Jafo.

Kipindi cha TUNATEKELEZA kinaratibiwa na Idara ya HABARI MAELEZO na kurushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na awamu hii inawashirikisha Mawaziri wote ambapo wanapata fursa ya kueleza utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Sera na program mbalimbali  zinazotekelezwa na Serikali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527