DREAMLINER YATUA MWANZA NA KIKOSI CHA SIMBA


Baada ya kukosekana angani kwa siku tatu mfululizo kuanzia Agosti 14 hadi 16, 2018 ndege ya Boeing 787-7 Dreamliner imeanza tena kukata anga na tayari imetua katika uwanja wa ndege wa Mwanza.

MCL Digital iliyopiga kambi uwanjani hapo tangu asubuhi imeshuhudia ndege hiyo ikitua saa 3:48 asubuhi leo Agosti 17, 2018.

Miongoni mwa abiria waliokuja na ndege hiyo ni pamoja na kikosi cha timu ya soka ya Simba Sports Club ambayo kesho inacheza mechi ya ngao ya hisani dhidi ya Mtibwa Sugar kufungua pazia ya ligi kuu ya Tanzania.


Akizungumza na MCL Digital kwa njia ya simu, Kaimu Meneja wa Uwanja wa ndege Mwanza, Julius Msofee amesema ndege hiyo yenye uwezo wa kubeba abiria 262 tayari imeruka kuendelea na safari kwa mujibu wa ratiba yake.


“Dreamliner imetua salama na tayari imeruka kuendelea na safari kwa mujibu wa ratiba. Miongoni mwa abiria waliokuja nayo ni wachezaji na viongozi wa timu ya Simba,” amesema Kaimu Msofee.


Ndege hiyo iliyozindua safari zake Julai 29, 2018 ilisitisha safari zake kati ya Dar es Salaam – Kilimanjaro – Mwanza tangu Agosti 14 kwa kile kilichoelezwa na Mkurugenzi Mkuu wa shirika la ndege nchini (ATCL), Ladislaus Matindi kuwa ni matakwa ya kiufundi ikiwamo kuangalia marekebisho ya suala la WiFi inayotakiwa kufanya kazi.

Na Jonathan Musa, Mwananchi
Chanzo - Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527