CCM KUAMUA HATMA YA MKUU WA MKOA WA MBEYA KUNG'ANG'ANIA UENYEKITI WA CCM IRINGA


Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole.

Baada ya kuwepo kwa mkanganyiko juu ya Mkuu mpya wa mkoa wa Mbeya Mh. Albert Chalamila kushika nyadhifa mbili ya Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Iringa na Mkuu wa mkoa wa Mbeya, CCM imesema suala hilo litaamuliwa na Kamati Kuu ya chama hicho.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Ndugu Humphrey Polepole ameongea na www.eatv.tv na kueleza kuwa kila kitu kipo kwa mujibu wa Katiba ya chama hicho hivyo suala la Albert Chalamila kuwa na kofia mbili litaamuliwa kwenye mkutano wa kamati kuu unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni.

''Kanuni ya uchaguzi ya CCM inaeleza bayana mtu mmoja kofia moja, lakini pia kanuni imetoa mamlaka kwa kamati kuu ya chama kumwezesha mtu mmoja kushika kofia mbili endapo itaona inafaa na kamati chini ya Mwenyekiti Ndugu Magufuli itakaa hivi karibuni na itaamua kama aendelee na kofia zote au moja'', - amesema.

Chalamila aliteuliwa hivi karibuni na Rais John Magufuli pamoja na viongozi wengine wa mikoa na wilaya ambapo jana kupitia mkutano wake na viongozi wa dini mkoa wa Mbeya aliweka wazi kuwa hawezi kujiuuzulu uenyekiti wa wa CCM mkoa wa Iringa labda apokee maelekezo kutoka kwa Rais ambaye amemteua.
Mwenyekiti CCM mkoa wa Iringa ambaye pia ni mkuu wa mkoa wa Mbeya Mh. Albert Chalamila (aliyesimama).

Chalamila sio kiongozi wa kwanza wa CCM kuwa na kofia mbili ambapo alitanguliwa na wengine kama Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi aliyeteuliwa na Rais Magufuli mwaka 2016 kuwa mkuu wa mkoa huo huku akiwa mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya. Hata hivyo, katika uchaguzi wa chama hicho mwaka jana, Zambi hakutetea kiti chake.

Kiongozi mwingine ambaye amewahi kushika nyadhifa mbili ni mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Kasheku ‘Musukuma’ ambaye alikuwa Mwenyekiti wa chama hicho mkoani Geita ambaye naye hakutetea nafasi hiyo katika uchaguzi wa mwaka jana.
Chanzo - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527