CAF YAWAFUNGIA WAAMUZI NANE

Shirikisho la soka barani Afrika CAF limewafungia waamuzi nane wa Ghana kuchezesha soka kwa kashfa ya rushwa.


Huo ni muendelezo wa kashfa ya rushwa iliyoibuliwa na mwaandishi wa habari za kiuchunguzi nchini Ghana, Anas Amereyaw Anas iliyoonesha waamuzi kadhaa wakipokea rushwa ili kufanya maamuzi ya upendeleo kwenye ligi kuu ya nchi hiyo.

Kwesi Nyantakyi, aliyekuwa rais wa shirikisho la soka la Ghana tayari alishasimamishwa na CAF. Katika kikao cha bodi ya CAF kilichokaa hivi karibuni kimewakuta na hatia waamuzi wengine nane.

Mwamuzi msaidizi wa FIFA, David Laryea amefungiwa maisha kuchezesha soka, walati huohuo waamuzi wengine, Reginald Lathbridge, Eric Nantierre, Cecil Fleischer na Dawood Ouedraogo wakifungiwa miaka 10.

Rungu hilo pia limewakuta mwwamuzi wasaidizi, Malik Salifu na Theresa Akongyam na mkurugenzi wa ufundi Joseph Wellington ambao wote wamefungiwa miaka 10. CAF pia imewasimamisha maafisa 14 kutoka sehemu mbalimbali barani Afrika na kutakiwa kuhudhuria katika kamati ya nidhamu ya shirikisho hilo.

Mwandishi Amereyaw Anas amekuwa maarufu katika eneo la Afrika magharibi kwa kazi yake ya kuendesha uchunguzi hasa katika masuala ya rushwa michezoni, ambapo katika uchunguzi wake mpaka sasa umesababisha viongozi kadhaa wa soka na waamuzi kuchukuliwa hatua ikiwemo kufungiwa .

Kigogo mwingine ambaye alikubwa na kashfa hiyo ni pamoja na mwamuzi wa Kenya, Aden Marwa ambaye alichaguliwa kuchezesha michuano ya kombe la dunia nchini Urusi kisha kuondolewa kwenye listi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527