KIKOSI CHA KUDHIBITI UNUNUZI HOLELA NA UTOROSHAJI MAZAO CHAKAMATA MALORI 14 KILWA


Jitihada za kikosi kazi maalumu cha kudhibiti utoroshaji na ununuzi holela mazao ya kilimo cha wilaya ya Kilwa mkoa wa Lindi,zimefanikisha kukamatwa kwa malori 14 yenye ufuta yanayoshukiwa yalikuwa yanasafirisha kinyume cha sheria.

Akieleza tukio hilo lililotokea jana,mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama,ambae ni mkuu wa wilaya hiyo,Christopher Ngubiagai alisema malori hayo yalikamatwa katika kizuizi cha Marendego kilichopo katika wilaya hiyo yakiwa safarini kwenda Dar-es-Salaam.

Alisema kikosi kazi hicho cha wilaya kikiwa kinatekeleza majukumu yake ya kila siku,ikiwa ni pamoja na kutembelea maghala na vituo vya ununuzi katika vyama msingi vya ushirika.

Alieleza kuwa kikosi hicho kilipata taarifa kutoka katika kizuizi cha Marendogo kwamba kuna malori yamekutwa na ufuta na baadhi yake yamekutwa hayana nyaraka halali za kununulia na kusafirishia zao hilo.

Ngubiagai ambaye aliongoza kikosi kazi hicho na kwenda kwenye eneo la tukio,alitaja baadhi ya makosa yaliyodhihirika baada ya kufanya ukaguzi na uchambuzi wa awali wa nyaraka hizo ulifanyika kizuizini hapo ni baadhi ya malori hayo kusafirisha zao hilo kwakutumia hati za kusafirishia mazao ya kilimo (Produce Delivery Note/PDN) zilizotumika na kutogongwa mihuri ya vyama vya msingi vya ushirika (AMCOS) kwenye baadhi ya nyaraka hizo na kusababisha hisia kwamba ufuta huo ulikuwa unatoroshwa baada ya kununuliwa visivyo halali. 

Alisema kwa mujibu wa mwongozo wa utaratibu wa ununuzi wa zao hilo katika mkoa wa Lindi kwa msimu wa 2018 unaohusu udhibiti wa ununuzi na usafirishaji zao hilo kwamba kamati za ulinzi na usalama za wilaya na ya mkoa zina wajibu wa kudhibiti vitendo vyote vinavyoweza kusababisha utoroshaji na ununuzi usiozingatia sheria hivyo wilaya hiyo inatekeleza mwongozo huo kwa vitendo. 

"Mwongozo huo unasema halmashauri za wilaya zitatumia sheria ndogo za ushuru wa mazao ambazo zimetungwa chini ya sheria ya fedha ya serikali za mitaa ambazo zilifanyiwa marekebisho mwaka 2017.Ndani yake kuna aina ya adhabu na yanayotakiwa kufanywa na watu kama hawa. Kwa kuzingatia hilo tunataka walipe ushuru wa halmashauri na walipe faini ya kiwango cha juu kilichopo kwenye sheria hiyo,"alisisitiza Ngubiagai.

Alibainisha kwamba kilo 295,349 zilizokamatwa zimerejeshwa na kuhifadhiwa kwenye maghala yaliyopo Nangurukuru wilayani humo huku akiweka wazi kwamba kilo 531,591 zinahofiwa zilipita bila kuwa na nyaraka halali kutokana uchambuzi wa awali wa nyaraka zilizopo unaondelea kufanyika.

"Kwa kuzingatia sheria ya fedha ya serikali za mitaa namba 290 tumebaini kwamba halmashauri zimepoteza takribani shilingi 44,653,626 ambazo ni tozo ya asilimia tatu ya bei ya sokoni ya shilingi 2,800 kwa kila kilo moja," alisema Ngubigai.


"Kwa kurejea mwongozo wa tozo mbalimbali za zao hilo kwa mwaka 2018 takribani shilingi 66,448,857 zimepotea,kikosi kazi kinaendelea kufanya chambuzi wa nyaraka kwa sababu baadhi nyaraka hizo maelezo yake yamejirudiarudia hali inayodhihirisha kwamba ununuzi holela na utoroshaji ulianza muda mrefu.

Aidha alishauri na kutoa wito kuwepo stakabadhi za malipo zinazotambulisha ufuta ulionunuliwa kutoka nje ya chama kikuu cha Lindi Mwambao ikiwemo unaotoka katika wilaya ya Ruangwa,jeshi la polisi liendelee kufanya uchunguzi ili kuwabaini wote waliotorosha ufuta ili wakamatwe,vyama vya ushirika vishirikishe halmashauri katika zoezi la ununuzi na ngazi ya mkoa iwe karibu na halmashauri ili kudhibiti hujuma katika ununuzi na usafirishaji zao hilo.

Malori yaliyokamatwa yamezuiliwa hadi uchunguzi utapokamilika na ikibainika yalikiuka kanuni,taratibu na sheria yatachukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527