KATIBU MKUU WA CCM AWATAKA WANANCHI WASIFANYE MAKOSA BUYUNGU

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi( CCM )Dkt, Bashiru Ally amewataka wananchi kuunga Mkono jitihada zinazofanywa na Serikali ya CCM ya kuwaletea maendeleo Wananchi bila kujali itikadi za vyama vyao.

Katibu Mkuu huyo alitoa kauli hiyo jana  katika kata ya Kiziguzigu wakati akimnadi mgombea ubunge jimbo la Buyungu kupitia CCM Christopher Chiza ambapo aliwaomba Wananchi kumchagua mbunge wa chama hicho kwa kuwa ana uzoefu mkubwa bungeni na anajua namna ya kwenda kuwasemea.

Aidha aliwataka wananchi wa wilaya ya Kakonko kuachana na wanasiasa waliofirisika wanaofanya siasa za ubaguzi kwa kuwagawa wananchi na wachague mgombea atakakwenda bungeni kuwatetea Wanakakonko na kuunga kusaidiana na serikali kuwaletea maendeleo.

"Niwaombe wananchi msifanye makosa leo tumekuja kwenu chama kilichopo madarakani kimemuamini Chiza awe mgombea wenu wa nafasi hii, nina uhakika ni kiongozi anayefaa na atafanya kazi yake kwa uaminifu, kosa mlilolifanya kipindi kilichopita msilirudie, niwaombe muendelee kukiamini Chama Cha Mapinduzi kwa kazi kubwa tunayoifanya," alisema Katibu Mkuu.

Kwa upande wake mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde  alisema wananchi wa Kakonko wanatakiwa kukaa chini na kupima mambo aliyoyafanya Chiza kipindi alichokuwepo bungeni na kujiridhisha kwamba ni kiongozi ambaye anafaa kupata nafasi hiyo.

Alisema Chiza ni kiongozi ambaye akisimamia jambo lazima lifanyike na ana uwezo wa kujenga hoja akiwa bungeni na ikafanyiwa kazi hivyo wananchi wanatakiwa kuwa makini katika uchaguzi wao.

Nae Mbunge wa Nzega mjini Hussein Bashe alisema Chiza ni kiongozi ambaye akiwepo bungeni ana busara sana na anajua kutafuta wawekezaji alisema wapo wanasiasa watakaokuja kuwadanganya wananchi na kuwapotosha ili wasipate nafasi hiyo wawapuuze.

"Tumeishi na Chiza muda mrefu bungeni ndio maana leo sisi wabunge tumeungana kuja kumuunga mkono tunajua utendaji kazi wake msidanganywe na mtu wananchi wa Kakonko mchagueni Chiza kwa maendeleo yenu nina uhakika hamtajutia hili", alisema Bashe.

Naye mgombea ubunge jimbo la Buyungu mhandisi Christopher Chiza aliahidi kushughulikia kero mbalimbali zikiwemo za maji na barabara.

Kada maarufu wa Chama cha mapinduzi Yusuphu Makamba anatarajiwa kuzindua rasmi kampeni za chama hicho leo jimbo la Buyungu wilayani Kakonko.
Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527