MEYA MANISPAA YA SHINYANGA AKABIDHI PAMPU YA MAJI YA KISIMA KIREFU KOLANDOTO


Mstahiki Meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadam amekabidhi pampu ya maji kisima kirefu kwa wananchi wa kitongoji cha Kisesa ( Zaire) kilichopo katika kijiji na Kata ya Kolandoto manispaa ya Shinyanga kwa lengo la kuwaondolea kero ya kutumia maji machafu.


Meya amekabidhi pampu hiyo leo Juni 21,2018 kwenye Ofisi za manispaa ya Shinyanga pamoja na mifuko 10 ya saruji kwa diwani wa kata ya Kolandoto Agnes Machiya kwa niaba ya wananchi wa kitongoji hicho ili kujenga kisima chao na kuwa katika hali ya usalama.

Mukadam amesema hivi karibuni alipofanya ziara kwenye kata hiyo na kufika kwenye kitongoji hicho cha Kisesa alikutana na wananchi wakikabiliwa na uhaba mkubwa wa maji safi na salama, na hivyo kuwahamasisha kuchimba kisima kirefu ambapo yeye ameamua kutoa msaada wa kuwawekea pampu ya kuvuta maji hayo kutoka chini.

“Mimi kama Meya wa manispaa hii nitaendelea kutatua kero za wananchi za uhaba wa maji safi na salama ,ambapo kazi kama hii nilishaifanya pia katika kata ya Chibe kwa kuwawekea wananchi pampu ya kisima cha maji, na leo nakabidhi tena Kolandoto,na hii ni moja ya utekelezaji wa ilani ya CCM ya kumtua ndoo mwanamke kichwani,”alisema Mukadam.

Aidha alitaja thamani ya pampu hiyo kuwa ni shilingi milioni 1.8, mifuko ya saruji laki 170,000/-= jumla ni Shilingi Milioni 1.9.

Aidha alitoa wito kwa wananchi kuilinda miundombinu hiyo idumu kwa muda mrefu ambayo itakuwa msaada kwao kwa kuwaondolea adha ya kutumia maji machafu. 

Naye Diwani wa Kata hiyo ya Kolandoto Agnes Machiya ambaye pi ni Naibu Meya wa manispaa hiyo ya Shinyanga, alipongeza juhudi za Meya huyo kwa kutatua kero za maji kwa wananchi na kubainisha kuwa wapiga kura wake hao walikuwa na shida ya maji safi na salama kwa muda mrefu na wamekuwa wakitumia maji ya mito na mabwawa.
Na Marco Maduhu - Shinyanga.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Kulia ni Mstahiki Meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadamu akimkabidhi pampu ya maji ya kisima kirefu katibu tawala wa wilaya ya Shinyanga Boniphace Chambi kwa niaba ya mkuu wa wilaya hiyo ya Shinyanga Josephine Matiro kwa ajili ya kutatua changamoto ya uhaba wa maji safi na salama katika kitongoji cha Kisesa kilichopo kijiji na Kata ya kolandoto- Picha na Marco Maduhu
Kulia ni Katibu tawala wilaya ya Shinyanga Boniphace Chambi akimkabidhi pampu ya maji ya kisima kirefu na mifuko 10 ya saruji Diwani wa Kata ya Kolandoto Manispaa ya Shinyanga Agnes Machiya ambaye pia ni Naibu Meya wa manispaa hiyo kwa niaba ya wananchi wa kitongoji cha Kisesa, msaada ambao umetolewa na Mstahiki Meya wa manispaa hiyo Gulam Hafeez Mukadam.
Mstahiki Meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadam Mwenye Shati ya Kijani akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wataalamu wa maji na afya, pamoja na Katibu tawala wa wilaya ya Shinyanga Boniphace Chambi mara baada ya kumaliza kumkabidhi pampu ya Maji Diwani wa Kata ya Kolandoto Agnes Machiya kwa niaba ya wananchi wake wa Kitongoji cha Kisesa.
Mstahiki Meya wa manispaa ya Shinyanga Gulam Hafeez Mukadam akizungumza mara baada ya kumaliza kukabidhi msaada huo wa pampu ya maji ya kisima kirefu na mifuko 10 ya Saruji, amesema ataendelea kusaidia wananchi kutatua kero za maji, kama Ilani ya CCM inavyosema ya kumtua ndoo kichwani Mwanamke.
Diwani wa kata ya Kolandoto manispaa ya Shinyanga Agnes Machiya ambaye pia ni Naibu Meya wa manispaa hiyo, akitoa shukrani kwa niaba ya wananchi wake, na kuahidi kwenda kuilinda miundombinu hiyo, ambayo itakuwa na faida ya kutatua changamoto ya kutumia maji machafu.
Pampu ya maji na mifuko 10 ya Saruji ikiwa kwenye gari mara baada ya kumaliza kukabidhiwa tayari kupelekwa kuwekwa kwenye kisima cha maji cha wananchi wa Kitongoji cha Kisesa kata ya Kolandoto

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527