MBWA WAZUA MVUTANO KWENYE KIKAO CHA MADIWANI

Uamuzi wa wataalamu wa mifugo kuwaua kwa kuwapiga risasi mbwa wote wanaozurura mitaani umepingwa katika Wilaya ya Siha na kusababisha baadhi ya viongozi wa kisiasa kutaka zoezi hilo lisitishwe na wanyama hao kupatiwa chanjo.

Katika Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo, baada ya Diwani wa Kata ya Karansi (CCM), Dancan Urassa aliitaka idara ya mifugo kuwaua kwa risasi mbwa wote wanaozurura mitaani kwa kukosa uangalizi, ili kuepuka mlipuko wa ugonjwa wa kichaa cha mbwa unaosababishwa na virusi vinavyoshambulia mfumo wa fahamu na ubongo.

Hata hivyo hoja hiyo, ilipingwa vikali na Diwani wa Kata ya Kirua (CHADEMA), Robert Mrisho, aliyedai kwamba hatua hiyo ni kwenda kinyume na haki za wanyama na ni ukatili dhidi ya wanyama.

“Mimi sikubaliani na hoja ya kuua mbwa kwa kuwapiga risasi, nadhani njia nzuri na inayokubalika ni kuwakamata na kuwapa chanjo ya kuzuia kichaa cha mbwa na ndio njia bora ya kwanza ya kulinda ustawi wa wanyama" amesema .

Ameongeza "Kama kuna zoezi hilo lisitishwe haraka na wapewe chanjo, ili kuepuka ukatili dhidi ya wanyama kwa sababu wanayo haki ya kuishi,” alisema Mrisho.

Baada ya mvutano huo, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Frank Kisinani ameunga mkono hoja ya Diwani wa Karansi na yeye akitaka uamuzi wa kuwapiga risasi ubaki kama ulivyo hata kama haki za wanyama zinakataza kuua wanyama.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527