Mwenyekiti wa UVCCM mkoa wa Kigoma Sylivia Sigula
Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoani Kigoma umepokea kwa masikitiko na huzuni taarifa za kifo cha aliyekuwa Mwenyekiti Mstaafu wa CCM Mkoa Kigoma Dkt. Walid Amani Kabourou aliyefariki jana /usiku wa kuamkia leo Jumatano,Machi 7,2018 katika hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam.
Katika salamu za rambirambi kutoka kwa Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa Kigoma Sylivia Sigula kwenda kwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa Kigoma Ammandus Nzamba , UVCCM wameelezea kusikitishwa kwao na kifo cha kiongozi huyo mkoani humo.
Sylivia amemuomba Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kigoma awafikishie salamu zao za zarambirambi na mkono wa pole kwa familia ya marehemu, ndugu na jamaa na kuwataka wawe na moyo wa subira na ustahamilivu katika kipindi hiki kigumu.
Aidha Mwenyekiti huyo wa UVCCM amemtaja marehemu Dk Kabourou katika maisha yake amekuwa kiongozi aliyetawaliwa na busara, hekima, maarifa mapana na mwenye upeo mkubwa katika medani za siasa na historia ambapo mara zote amekuwa zaidi ya mwalimu kwa vijana.
"Chama chetu kimepoteza kiongozi wake bora, msikivu na mjuzi katika masuala ya siasa na maendeleo ya demokrasia .Tunamuomba mungu mtukufu ampokee, amsaheme dhambi zake na amuweka mahali pema peponi",ameeleza Sylivia katika salamu zake za rambirambi.
Hata hivyo Mwenyekiti huyo wa UVCCM amesema jumuia yake mkoani humo itaendelea kujifunza na kuyaenzi mambo yote mema na mazuri yaliyokuwa yakifanywa na Dkt. Kabourou wakati wa uhai wake na jinsi alivyokuwa mahiri katika kujenga hoja na kujibu mapigo ya kisiasa.
Pamoja na salamu hizo za rambirambi, Sylivia amesema mwili wa marehemu Dr. Walid Kabourou utasafirishwa kutoka Dar es salaam kuelekea Kigoma Kesho saa nne asubuhi.
Mazishi yanatarajiwa kufanyika siku ya Ijumaa,tarehe 9 Machi 2018 katika makaburi ya Kipampa shule ya Ujiji.
Msiba upo nyumbani kwa marehemu huko Bagwe, Kigoma Mjini
Inna lilahi wa Inna Ileiyhi Rajiun .
Imetolewa na:
Mwenyekiti wa UVCCM mkoa wa Kigoma Sylivia Sigula